Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2021-02-04

Name

Aida Joseph Khenani

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, dhana ya Serikali ya kutenga maeneo na kusimamia hifadhi zilizopo nchini kwetu ilikuwa ni kulinda rasilimali za nchi yetu. Sote tunajua wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi mbalimbali ni wahifadhi namba moja, jambo ambalo kwa sasa limebadilika kulingana na watendaji aidha ni wachache, kulingana na mambo yanayofanyika hivi sasa.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, natambua kumekuwa na kelele nyingi na malalamiko mengi kutoka kwa sisi Wabunge kwa wananchi wetu. Leo wananchi wanaozunguka hifadhi, wanaoshughulika na shughuli za kawaida ikiwemo kilimo, ufugaji na uvuvi, imekuwa changamoto ya kupigwa, kunyanyaswa, kunyang’anywa mifugo, jambo ambalo linakwenda kuondoa ile dhana ya wao kuwa wasimamizi wa hizi hifadhi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, miongoni mwa changamoto zinazopelekea vurugu hizo ni mipaka inayobadilishwa kila siku na mipaka mingine ambayo haieleweki, kwa maana ya kwamba havijawekwa vitu ambavyo vinaonesha alama kwamba hapa ni mpaka.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa haraka wa kwenda kupitia upya maeneo hayo ambayo yanasababisha migogoro kwa wananchi wetu ili mipaka hiyo ieleweke; na pia wanapokwenda kutengeneza au kupima hiyo mipaka, iwe shirikishi. Napenda kujua Serikali ina mpango gani wa haraka?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunayo changamoto ya uwepo wa migogoro kati ya wananchi waliopo pembezoni mwa Hifadhi zetu za Taifa, mapori tengefu ambayo yameweka ukomo wa wananchi hao kuingia kwenda huko. Migogoro hii mara nyingi imetokana na kutoeleweka kwa uwepo wa mipaka kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili Serikali imefanya jitihada kubwa; moja, ni kutoa elimu ya wananchi walioko kwenye vijiji vilivyo karibu na mipaka hii; kwanza kutambua ukomo wa mipaka ya Hifadhi hizo za Taifa na maeneo ambayo wananchi wanaishi huku wakiendelea kupata huduma za kijamii kwenye suala la uchumi na mambo mengine, kwa mfano kilimo, mifugo na shughuli nyinginezo.

Mheshimiwa Spika, uwepo wa migogoro kwenye maeneo haya ni pale ambapo kama Mbunge alivyosema, mipaka haieleweki. Jukumu hili tumeshawapa Wizara ya Maliasili kuhakikisha kwamba wanapitia ramani zilizopo na kwenda kila mahali palipo na migogoro ili kuondoa migogoro hiyo ili wananchi waweze kuishi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameonesha kwenye Jimbo lake pia kuna migogoro ya hiyo, ndiyo sababu amekuja na swali hili. Kwa hiyo, nimuagize sasa Mheshimiwa Waziri wa Maliasili kufika Nkasi Kaskazini kuona mgogoro huo ili kutatua tatizo hilo kwa kubainisha vizuri mipaka na kuweka alama zinazoonekana zitakazomwezesha mwananchi kutokuingia kwenye eneo hilo ili kuepusha migogoro ambayo ipo. Nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba maeneo haya ya hifadhi, lakini pia mapori tengefu yanaendelezwa kwa malengo yaliyowekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunatamani kuona wananchi walipo pembezoni wakiendelea na maisha yao, shughuli zao za kijamii, kilimo, mifugo na indelezwe lakini pia kwa kuzingatia mipaka ile. Kwa hiyo, kama ni tatizo la mipaka, tayari Mheshimiwa Waziri atakuwa amepokea kauli yangu na agizo langu, aende Nkasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo Nkasi tu, na popote pale ambako kuna migongano kati ya wananchi na mipaka ili tubainishe kwa uwazi kabisa na sasa zoezi hilo liwe shirikishi; wananchi walioko jirani washirikishwe na maafisa walikuwepo pale washirikishwe, wafanye kazi kwa pamoja na kila mmoja afanye kazi yake kwa amani na watu wajipange, waongeze uchumi wao kupitia fursa zilizopo kwenye maeneo yao. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister