Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2021-02-04

Name

Joseph Anania Tadayo

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Primary Question

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa Serikali imetumia nguvu nyingi sana katika kupambana na uvuvi haramu na kulinda hifadhi zetu na kama sehemu ya mafanikio ya juhudi hizi idadi ya wanyamapori imeongezeka na katika maeneo mengine wanyamapori hawa wamesambaa na kuingia katika makazi ya watu na hivyo kuathiri sana maisha ya watu na shughuli za uzalishaji. Kwa kuwa tatizo hili sasa limeonekana kuwa la kudumu, Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya suluhisho la kudumu la tatizo hili? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tadayo, Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali hili linafanana sana na swali ambalo mwanzo nimetoa ufafanuzi wake kwamba yako maeneo yana migogoro kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi. Swali la awali lilikuwa linazungumzia ule mgongano wao na hili linzungumzia wanyamapori walioko.

Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo haya tuliyoyahifadhi yana hawa wanyamapori na maeneo haya ya wanyamapori pia tumeendelea kuwahifadhi na kutoa tahadhari kwa wananchi walioko jirani na maeneo haya. Mkakati wa kuzuia wanyamapori hawa kuja kwenye makazi ya wananchi upo na unaendelea pale ambapo kwanza tumetoa elimu kwa wananchi wanaokaa karibu na maeneo haya ya wanyamapori kuwa na tahadhari. Wanapofanya shughuli zao wasiingie kwenye eneo la wanyamapori, pia tumewawekea buffer ya mita kama 500 ambazo wao wananchi walioko huko hata wanapoingia eneo hili lazima wawe na tahadhari ya kutosha. Tunaamini wanyama walioko kwenye lile pori wanaweza kuja mpaka kwenye mpaka wa kijitanua kidogo wanaingia kwenye hili eneo la mita hizi 500, wanaweza wakazunguka hapo na kurudi. Inapotokea wakija huku sasa Idara ya Maliasili kupitia kikosi chao cha wanyamapori tumekiweka maeneo yale ambayo wanyamapori huwa wana tabia ya kutoka na kurudi huku kwa ajili ya kuwazuia kurudi kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, jambo hili tunalifanya kwa kushirikisha pia vijiji vyenyewe, tunawapa elimu tunaanzisha ulinzi wa kijiji ambako pia ikitokea hilo nao wanasaidia kuwarudisha. Bado tunao wanyama wanatoka wanakuja lakini bado tumeendelea kuimarisha vikosi vyetu kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo yana wanyamapori wanaotoka sana kuweka kambi dogo la kuhakikisha kwamba wanarudishwa kwenye maeneo hayo na makambi hayo tumeamua tuyaweke katika maeneo yote ambayo tunaona wanyama kama tembo ambao wameongezeka sana kwa sasa waweze kudhibitiwa.

Mheshimiwa Spika, nimeliona hili pia nilipokuwa nafanya ziara wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, nimeona pia nikiwa Bariadi Mkoani Simiyu, nimeenda pia hata Tarime na maeneo mengine ambayo nimepita, nimepata malalamiko haya na tumeshawasiliana na Wizara ya Maliasili kujiandaa vizuri kwenye maeneo haya. Kwa hiyo, tumeshaanza kusambaza vikosi vyetu, kulinda maeneo hayo ili pia wananchi wasiweze kusumbuliwa.

Mheshimiwa Spika, wito kwa wananchi walioko kwenye vijiji ambavyo viko karibu na maeneo ya hifadhi, wasiingie sana kwenye mapito ya mara kwa mara ya wanyama. Tunao wanyama kama tembo ambao wao wana mapito yao miaka yote. Kwa hiyo, maeneo hayo kwa sababu tunaishi kwenye vijiji hivyo, tunayafahamu. Ni muhimu kuwa na tahadhari kwenye maeneo haya ya mapito ili tusije tukawa tunaingiliana na hawa wanyama, lakini bado mkakati wetu ni ule ule. Kwa hiyo, tushirikiane pamoja kuhakikisha kwamba tunawahifadhi wanyama wetu na madhara ambayo yanajitokeza pia tunaendelea kuyadhibiti ili yasiweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mkakati wa kudhibiti hatari hii unaendelea chini ya maliasili kwa kuweka makamanda kwenye maeneo hayo na kila wilaya iliyoko kwenye mpaka tuna kitengo hicho ambacho pia kinafanya kazi hiyo kubaini kwenye mipaka yake kwamba wakati wote tunakuwa salama. Lengo ni kuwalinda wananchi wanaoendelea na shughuli zao, lakini pia kuwalinda wanyamapori ambao pia na wao watatupatia tija kwa shughuli za kitalii na uhifadhi wa wanyama wetu kwa ajili ya sasa na vizazi vijavyo. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister