Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2021-02-11

Name

Neema Kichiki Lugangira

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, swali langu ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na tatizo kubwa la masoko ya mazao yetu hata kama tunazalisha kwa ubora wa juu. Je, Serikali iko tayari kupeleka wataalam wake nje ya nchi na hasa kwenye nchi ambazo zimefanikiwa ili kujifunza namna bora ya usimamizi wa masoko yetu? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lugangira, Mbunge wa Mkoa wa Kagera, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la kutafuta masoko kwenye mazao yetu lakini pia Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mpango wa Serikali wa kuwapeleka wataalam wetu nje ya nchi kujifunza kutafuta masoko. Sina uhakika sana kama alikuwa anataka kusisitiza kuwepo kwa masoko au suala ni kupeleka wataalam kujifunza masoko. Hata hivyo, Serikali yetu inatambua na inao mkakati ambao sasa tunaendelea nao wa kuzalisha mazao mengi ya chakula na biashara. Kwenye mazao yote ya biashara tumeendelea kuboresha kupata masoko ya ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuwapatia nafasi nzuri wakulima wetu kuuza mazao yao vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini pia inapoingia kwenye utaalam wa kutafuta masoko muhimu zaidi ni kujua kama mazao tunayozalisha tuna masoko huko nje? Tunachokifanya sasa kila zao kupitia Balozi hizi nazo tunazitumia kutangaza mazao tuliyonayo ndani ya nchi ili tuweze kuyauza kwenye nchi wanazotumia mazao hayo. Zoezi hili linaendelea na tunapata wateja wengi kuja kununua mazao yetu na hali hiyo imesababisha masoko yetu kuimarika.

Mheshimiwa Spika, muhimu kwetu sisi ni kutafuta mfumo mzuri unaowezesha mazao haya kujulikana na kuyauza na tupate bei nzuri. Kama ambavyo sasa ndani ya nchi tumeweka Mfumo wa Stakabali Ghalani ambao unakusanya mazao pamoja na kuwaalika wanunuzi kila mmoja anatamka atanunua zao hilo kwa shilingi ngapi kwa kilo, yule mwenye bei ya juu ndiye ambaye tunampa fursa ya kununua. Kwa hiyo, huo ni mfumo wa uuzaji wa mazao yetu ambao tumeuandaa na tutapata bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia Serikali tunao mpango wa kutafuta masoko kwenye nchi ambazo zinazohitaji mazao hayo. Juzi hapa nilikuwa na Wabunge wa Mkoa wa Rukwa wakiomba Serikali iwasaidie kutafuta masoko ya mazao yanayolimwa Mkoani Rukwa kwa nchi za Zambia, Rwanda na Burundi. Kwa hiyo, kazi ambayo Serikali inafanya sasa ni kuwasiliana na nchi ambazo ni walaji wa mazao haya ili kuhakikishia kuwa mazao haya yanapolimwa na kuvunwa tunayapeleka kwenye nchi husika. Hiyo ni njia pia ya kupata soko zuri la mazao yetu.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali kwa sasa tunaendelea kujenga masoko ya kimkakati, masoko ya kikanda, ambayo tunayajenga pembezoni mwa nchi yetu ili kukaribisha ndugu zetu walioko jirani kuja kununua. Miezi mitatu iliyopita nilikuwa Mkoani Kilimanjaro, nimekwenda pale Horohoro, tunajenga soko kubwa sana ambalo pia wananchi wa maeneo hayo wakizalisha mazao yatawekwa hapo, wa nchi jirani wote watakuja hapo. Kwa hiyo tunawapunguzia ugumu wa kuingia mpaka huku ndani kutafuta mazao hayo badala yake tunawa-allocate kwenye masoko yale.

Mheshimiwa Spika, mwezi mmoja uliopita pia nilikuwa Mkoani Kigoma kule Kagunga. Tumejenga soko zuri sana. Kwa hiyo tunawakaribisha ndugu zetu wa Burundi na Rwanda kuja kununua pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajenga soko lingine kubwa sana Mkoani Kagera pale Nyakanazi. Lengo letu wale wote kutoka Kongo, Rwanda watakuja pale Nyakanazi kwenye soko letu lile la zaidi ya bilioni 3.5 ili wapate bidhaa. Kwa hiyo muhimu kwetu sisi ni kuweka mkakati wa namna gani mazao yetu yaliyoboreshwa yaweze kupata thamani kubwa kwa lengo la kumfanya mkulima aweze kupata tija kwa kazi ya kilimo anayoifanya. Kwa hiyo Serikali inaendelea na maboresho haya, Waheshimiwa Wabunge kama mna mawazo mengine ya kuboresha masoko, tunawakaribisha ili Serikali iweze kuimarisha upatikanaji wa mazao haya na iweze kuuza mazao haya kwa bei nzuri sana. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister