Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2022-11-03

Name

Aida Joseph Khenani

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, lakini nashukuru kwa kauli ya Serikali ambayo imetolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili la uvalishaji hereni kwa ng’ombe lilianza katika Mkoa wa Rukwa, Wilaya Nkasi, na ikafikia mahali mpaka kutishwa kwa wafugaji, na mimi Mbunge nikalazimika kwa sababu ilikuwa ni kauli ya Serikali, nikapita kuwahamasisha wafugaji kutii maagizo ya Serikali na wakatoa hiyo fedha ya shilingi 1,750. Leo kuna maeneo ambayo yalikuwa hayajafikiwa; kwa kuwa ni utaratibu mzuri mlileta ninyi upigaji chapa siyo wafugaji, Serikali ilitoa hayo maagizo na wafugaji wakalipa, leo likaja agizo lingine la uvalishaji hereni wametii.

Mheshimiwa Spika, naomba kujua, kwa kuwa ni nia njema ya Serikali, kwa wale ambao walikuwa tayari wameshalipa hiyo fedha, itakuwaje ili na wao wajione ni sehemu ya wafugaji wengine wa Tanzania?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatujasitisha malipo, tumesitisha zoezi hili ambalo linalalamikiwa ili kuipa nafasi Serikali kupitia Wizara ya Mifugo kufanya tathmini ya mapungufu ya kanuni iliyowekwa ili kuweza kufanikisha zoezi hili vizuri kwa kushirikisha na wadau. Kama kutakuwa na maamuzi mengine ndani ya Wizara ya kupunguza bei, fedha, itakuwa ni baada ya mjadala huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa sasa tumesitisha tu zoezi lenyewe kuendelea, kwa sababu tangu sheria imewekwa mwaka 2010 na kanuni zake mwaka 2011, kati ya mifugo milioni 45 ni mifugo milioni tano tu mpaka leo kuanzia mwaka 2011 ndiyo imefanikiwa kufikiwa. Kwa nini? Maana yake kuna tatizo. Kama tungetekeleza inavyotakiwa leo tungefikia angalau nusu ya mifugo yote nchini kuwekwa hereni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumesema tunasitisha kwa muda wa miezi mitatu, ili kuipa nafasi Wizara kukaa ndani ya Wizara yenyewe, kupitia kanuni zao kuona wapi kuna dosari zilizosababisha kutofanikiwa kupata mifugo mingi zaidi, lakini kupitia hayo malalamiko ambayo yanawafanya wafugaji au kukwepa au kutoshiriki vizuri au kujiunganisha vizuri na watendaji walio kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ambao ndio wanatakiwa kuwatambua watu wao kila Wilaya ili sasa kuweka mfumo mzuri unaowezesha kufikia hatua nzuri zaidi na kuondoa manung’uniko yanayotokana na utekelezaji ambao unaonekana si mzuri.

Mheshimiwa Spika, baada ya januari, sasa hayo mambo yote, maazimio yote yatakayokuwa yamefikiwa, ili waweze kufanya vizuri wakati wa utekelezaji yataanza kuanzia tarehe 1 Februari, 2023. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister