Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 21 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2022-05-12

Name

Rose Cyprian Tweve

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri Mkuu ugonjwa wa malaria unasababisha vifo vya Watanzania wengi hususan wanawake wajawazito na watoto. Naishukuru Serikali iliona tatizo na wakaamua kufanya investment kubwa pale Kibaha, takriban Bilioni 46 kujenga kiwanda cha viuadudu na ikasaini mkataba na NDC kwa makubaliano kuwa watanunua zile dawa na kusambaza katika maeneo yote nchini ili tuweze kutokomeza ugonjwa huu lakini haijafanya hivyo.

Kutokana na takwimu kutoka Mpango wa Kudhibiti Malaria Nchini tunatumia takribani Bilioni 108 kwa mwaka kufanya warsha na matamasha mbalimbali na preventive measures kama net kupambana na ugonjwa huo.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu nataka kujua mkakati wa Serikali kuhakikisha tunasaini mkataba tena na NDC wa kununua na kuhakikisha tunasambaza dawa hizi nchini kuhakikisha tunatokomeza janga hili ambalo linapoteza maisha ya Watanzania wengi. Nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tweve, Mbunge wa Mkoa wa Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu imefanya uwekezaji mkubwa sana pale Kibaha Mkoani Pwani, kwa kujenga kiwanda kikubwa sana kinachotengeneza viuadudu na ili kurahisisha masoko, Wizara ya Afya pamoja na Ofisi ya Rais - TAMISEMI, zimeingia mkataba wa kununua viuadudu na kuvisambaza kwenye hospitali zetu, Vituo vya Afya na hospital za Wilaya, Zahanati pia maeneo kama shule na taasisi zote ambazo zinakusanya vijana wengi na kuna tatizo la mbu. Kama sehemu ya awali ya soko mbali ya soko ambalo tunauza pia nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, utaratibu huu tuliingia mikataba ya kwamba kiwanda kile moja kati ya mteja atakuwa ni Serikali yenyewe kupitia Wizara zote mbili ili kukabiliana na tatizo la malaria inayosababishwa na mbu. Ni kweli kwamba Serikali inasimamia mauzo ya dawa hizo ndani na nje ya nchi, ziko Halmashauri ambazo bado hazijatekeleza wajibu wake wa kwenda kuchukua viuadudu, lakini baadhi ya hospitali ambazo ziko chini ya Halmashauri hazijapata huduma hiyo kupitia Halmashauri hizo. Mpango wa Serikali katika hili ni kuhakikisha kwamba tunawasisitiza Wakurugenzi wa Halmashauri kununua viuadudu vile ili wapulize kwenye maeneo ya makazi ya wananchi kupunguza kiasi cha mbu ili kupunguza ugonjwa wa malaria. Kwa hiyo, nachukua wazo lako na swali lako kama ushauri kwa Serikali tuimarishe mikataba, tupitie mikataba ili tuweze kusambaza dawa ile itusaidie: -

(i) Itapunguza tatizo la malaria inayosababishwa na mbu;

(ii) Tunaimarisha soko ambalo tunaliendesha kupitia uwekezaji mkubwa wa fedha ambazo umezitamka Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, hivyo, naomba nitoe wito kupitia swali hili kwa Halmashauri zote nchini lakini na hospitali za Mikoa zilizo chini ya Wizara ya Afya, kuhakikisha kwamba tunanunua viuadudu vinavyozalishwa kwenye kiwanda chetu ambacho Serikali na yenyewe ina hisa ili tuweze kupuliza kwenye makazi ya watu, maeneo ya jumuiya, tuweze kuua mazalia umbu na tuwe salama ugonjwa wa malaria ambao unasabishwa na mbu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo utaratibu na mkakati wa Serikali kwenye eneo hili. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister