Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 26 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2022-05-19

Name

Esther Nicholus Matiko

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka 2014 tulitunga Sheria ya Tozo ya Ujuzi na Maendeleo ambapo mwajiri wa sekta binafsi wenye wafanyakazi zaidi ya kumi walitakiwa kuchangia asilimia nne kwa mujibu wa kifungu cha 14 cha VETA. Lakini asilimia mbili zilielekezwa kwenda kwenye Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu.

Kwa kuwa sasa Serikali imejenga VETA nyingi nchini; na kwa kuwa ofisi yako sasa hivi imetoa fursa kwa vijana wengi kuweza kujiunga na mafunzo haya ya muda mfupi ili waweze kujiajiri na kuajiriwa.

Ni kwa nini sasa Serikali isione ni muda muafaka wa kurejesha ile asilimia mbili ile iliyopelekwa kwenye bodi ya mikopo iweze kurudi VETA ili waweze kutumia kukopesha wanafunzi hawa vifaa ambavyo watajifunzia na baadaye waweze kuondoka navyo kwenda navyo mtaani vya kuanzia kazi? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulitunga sheria inayotengeneza mgao wa fedha ambazo pia tungependa tuzione zikitumika kwenye vyuo vyetu vya elimu hasa kwenye ufundi stadi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mpango wa Serikali utakaowezesha vijana wanaohitimu VETA baada ya kuwa tumejenga VETA nyingi nchini namna ya kuwasaidia wanaohitimu ili waweze kuanza vizuri.

Mheshimiwa Spika, kimsingi Serikali imeanza kuimarisha sekta hii ya ujuzi kwa utaratibu, mwanzo tumeanza kujenga VETA na tulianza kujenga VETA kila mkoa, kazi ambayo tumekamilisha siku chache zilizopita; na mimi nimepata nafasi ya kupita mikoa mingi kuona maendeleo ya ujenzi; lakini pili tumeanza na programu ya ujenzi wa VETA kila wilaya zoezi ambalo sasa linaendelea. (Makofi)

Msimu uliopita tulipata fedha, Waheshimiwa Wabunge mlipitisha bajeti ya kujenga VETA 28 kazi ambayo inaenda mwishoni ili pia tuweze kujenga VETA nyingine.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme tunaenda kwa awamu, tumeanza na ujenzi wa miundombinu, lakini mbili tunatoa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, halafu tuje tuone sasa tuna idadi gani ya wanafunzi wanaohitimu, tuweze kutenga fecha pamoja na hiyo tozo ambayo pia tunatoza na ile asilimia tunayoitenga tuiingize kwenye mpango huo ili kutoa vifaa vitakavyowezesha kijana huyu anayehitimu kuanza mafunzo yake na stadi yake mara tu anapohitimu. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kulifanyia kazi jambo hili ili kuona hawa vijana wetu wanaoingia kwenye vyuo hivi kwa ajili ya kupata ufundi stadi anapomaliza anaanza kazi moja kwa moja.

Kwa hiyo kadri tunavyoendelea Wizara ya Elimu ambayo ndiyo inashughulikia elimu ya ufundi kupitia VETA itaendelea kuratibu na kuomba fedha zaidi na tunashukuru mmetupitishia bajeti ya Wizara ya Elimu katika sekta mbalimbali ikiwemo kwenye eneo la ujuzi, ili tuweze kuhakikisha kwamba vijana wa Kitanzania wanakuwa na ujuzi katika fani mbalimbali ambazo wao wanazihitaji ziwasaidie pia kwenye kujitafutia ajira au pia wao wenyewe kuwaajiri wengine, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister