Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 26 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2022-05-19

Name

Stella Ikupa Alex

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu ninatambua changamoto kubwa iliyopo ya ajira kwa vijana wetu, changamoto ambayo ni ya kidunia, lakini nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa juhudi kubwa ambazo imeendelea kuzichukua kuhakikisha kwamba vijana hawa wanaweza kujiajiri ama kuajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri Mkuu Serikali sasa inaonaje inapokuwa inatoa kibali cha ajira na kuzitangaza ajira ikawepo asilimia fulani ambayo itakuwa ni maalum kwa ajili ya vijana wenye ulemavu wenye sifa zinazotakiwa. Tofauti na ilivyo sasa hivi ambapo vijana hawa wamejikuta wanaomba ajira na kukosa na hivyo kuendelea kupelekea ugumu wa maisha kwao na hasa ikizingatiwa kwamba ulemavu na gharama? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ikupa, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu kwenye mfumo wetu wa ajira, utaratibu ambao pia unawatambua wenzetu wenye mahitaji maalum ambao pia wanaomba ajira kwenye eneo husika, tumeunda Tume, Tume inaitwa Tume ya Ajira ambayo ipo chini ya Ofisi ya Rais Utumishi, na tumejiwekea kanuni ambayo pia Tume ya Ajira inasimamia kanuni hii na pia tumetoa maelekezo kwenye sekta zote za ajira kwamba kila panapokuwa na nafasi ya ajira lazima tutenge asilimia tatu kati ya wajiriwa 20 iwe ni kwa ajili ya walemavu. Kwa utaratibu huu ambao tunaendelea nao sasa umewezesha wenzetu wengi wenye ulemavu kupata ajira kwenye sekta mbalimbali, muhimu ni kuwa na zile sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna maeneo ambayo pia hata kama hana sifa, lakini ana uwezo na anaweza akafanya kazi hiyo, basi Tume huwa inatoa fursa ya kuweza kuingia kwenye ajira na maelekezo ambayo tumeyatoa kwenye eneo hili ndugu zetu wenye ulemavu wanapata nafasi ya awali hata kwenye interview (kwenye mahojiano) wao wanaanza kwanza wanakamilisha alafu wengine wanafuata. Hii yote nikutambua wenzetu ili na wao pia waweze kuingia kwenye mfumo wa ajira.

Mheshimiwa Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Ikupa kwamba Serikali kupitia utaratibu huu inaendelea kuwahakikishia wale wenzetu wote wenye mahitaji maalum au wenye ulemavu kwamba pindi tunapotoa nafasi za ajira na wao pia watapata fursa ya kuwa sehemu ya watakaoajiriwa na wote mnaona kwenye sekta mbalimbali mnaona waajiriwa wapo, hata kwenye teuzi za Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wetu ametambua hili amefanya uteuzi kwenye ngazi mbalimbali Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, Maafisa mbalimbali kwenye sekta zote, hii maana yake ni nini; kuonesha kwamba Serikali inatambua uwepo wa ndugu zetu wenye ulemavu ambao pia wanao uwezo mkubwa wa kufanya kazi kuliko hata sisi ambao tuko imara kwenye viungo vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka niwahakikishie wale wote ambao wangetamani kuomba nafasi za ajira Serikalini ambao ni walemavu wajitokeze kila wanaposikia ajira kwa sababu fursa ipo na inatekelezwa kupitia taasisi zote zinazoajiri, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister