Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 26 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2022-05-19

Name

Esther Edwin Maleko

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kumuuliza Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mikoa takribani 15 ya Tanzania ikiwemo Kilimanjaro, Kagera, Tanga, Ruvuma na mingineyo uchumi wake unategemea sana zao la kahawa, lakini zao hili halina ruzuku.

Ni nini msimamo wa Serikali kuhakikisha zao hili linapata ruzuku kama ilivyo kwa mazao mengine ya kimkakati? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Malleko, Mbunge Viti Maalum Mkoa wa Kilimanjaro kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kahawa ni miongoni mwa mazao yanayotegemea kupandisha uchumi kwenye maeneo mbalimbali hasa kwenye mikoa ambayo Mheshimiwa ameitaja; na mimi juzi nilikuwa Mkoani Kagera kushughulikia zao hilo hilo, lakini pia jana tumekamilisha bajeti ya Wizara ya Kilimo na limechangiwa sana na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa juu ya ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upo mkakati wa Serikali kutoa ruzuku kwenye mazao mbalimbali ikiwemo kahawa na ruzuku inategemea sana kwenye zao hilo mahitaji yake makubwa kwa sababu kila zao lina mahitaji yake, lakini tunajua tuna suala la mbegu au miche wakati mwingine, lakini pia tuna madawa kwa maana ya pembejeo madawa, mbolea lakini pia namna bora ya kulisimamia zao hili hata maghala nayo pia tunaweza kuweka ruzuku kama alivyosema Waziri wa Kilimo jana. Zao la kahawa linalolimwa Kagera na kule Kilimanjaro kila eneo linategemea na mahitaji yao na hayo mahitaji ndio tunayoyafanyia ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano juzi nilipokuwa Kagera Vyama Vikuu vya Ushirika vilikuwa vinazungumzia wakulima wao kwamba kuna umuhimu wa kuongeza ruzuku kupata miche, lakini pia kuna tatizo la upungufu maghala na wanahitaji ruzuku kwa ajili ya maghala. Kwa hiyo unaweza ukaenda Mbinga nilishakwenda Mbinga wakati tunasimamia zao hili kule sehemu kubwa ilikuwa ni kupata ruzuku ya kupata mbolea kwa sababu Mbinga bila mbolea huwezi kukuza zao hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ruzuku inategemea na mahitaji ya zao na eneo hilo kwa hiyo Serikali imeweka utaratibu wa kutoa ruzuku na kwenye kahawa kama kule Kagera tumetoa ruzuku kwenye miche kupitia taasisi ya utafiti ya TACRI. Lakini pia tumeshakubaliana na Waziri na Waziri ameshaahidi kule Kagera kujenga maghala ambako pia tunaanza na mfumo wa masoko kupitia stakabadhi ghalani ambayo inahitaji kuwa na maghala. (Makofi)

Kwa hiyo ruzuku huko Mkoani Kilimanjaro na maeneo mengine tutakapokuja tutajua mahitaji ni nini na tutaona uwezo wa Serikali na mpango ambao tumeweka ruzuku basi tutatoa ruzuku kutegemea na eneo hilo na mahitaji ya zao hilo; huo ndio utaratibu ambao tunautumia kwenye mazao yetu karibu yote. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister