Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 26 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 8 2022-05-19

Name

Abdulaziz Mohamed Abood

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Mjini

Primary Question

MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kuna upimaji wa ardhi na maeneo mbalimbali yenye migogoro ya ardhi ikiongozwa na Wizara nane, sehemu nyingine ambazo zinapimwa ni maeneo ambayo yapo mbali na vyanzo vya maji nchini, imeleta taharuki kubwa kwa wananchi katika upimaji huu kiasi ambacho wananchi wanajua wanabomolewa nyumba zao nchini katika taharuki hii ya upimaji katika maeneo ya maji ya upimaji wa ardhi.

Je, Serikali ina kauli gani kwa wananchi kuondoa taharuki hii?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, swali linarudi tena kwa sura nyingine la migogoro kwenye maeneo, lakini natambua mara kadhaa nimekuwa nikipita Morogoro na Mheshimiwa Mbunge mara kadhaa amekuja na wananchi wanaotoka kwenye eneo lake hasa kule Mindu wakizungumzia ile amri ya ujenzi wa makazi umbali wa mita 60 na zaidi ya 60 na kule ilikuwa mita 500 kulikuwa na mgogoro wa aina hii.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeeleza awali kwamba ile timu ya Mawaziri ambayo inaratibu migogoro ya kitaifa na kwamba Serikali imeweka utaratibu wa kutatua migogoro kulingana na ukubwa wa migogoro na ngazi ambazo tumezipanga kutoka ngazi ya Kijiji, Kata, Wilaya, Mkoa na hatimaye Taifa kupitia timu yetu ya Mawaziri. Mgogoro ambao Mheshimiwa Abood mara kadhaa amekuwa akiusimamia na kuwasemea wananchi wake wa kule Mindu, bado kazi tunaendelea kuifanya na tunashirikiana na Ofisi ya Mkoa ili kuhakikisha mgogoro wa aina hii popote unapotokea ikiwepo na hapo Mindu tunaisimamia kwa karibu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutakapoona sasa kuna umuhimu wa kuleta timu ya Mawaziri wanane tutawaleta Mheshimiwa Abood pale Mindu ili kukaa na wananchi, kuwaelimisha na kuona namna nzuri ya kuwawezesha kufanya shughuli zao za kijamii ikiwemo na kilimo na hasa eneo lile.
Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Abood swali lake hili ambalo amelizungumza kwa ujumla jumla lakini kwakuwa na mimi nimeshashughulikia tatizo la Mindu pale Morogoro niendelee kumhakikishia kwamba tunashughulikia na tutatatua tatizo lile kwa haraka sana. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister