Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 31 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2022-05-26

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imetimiza sera muhimu ya uwekezaji nchini na hasa katika sekta ya madini. Katika kutimiza azima hiyo, wawekeza wamekuwa wakichukua maeneo ya watu maeneo kama kule Kabanga, Sumbawanga na kule Nyamongo, lakini maeneo hayo imechukua muda mwingi sana ama kuchelewa kulipwa au kutokulipwa kabisa fidia za wananchi.

Mheshimiwa Spika, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wananchi ambao maeneo yao yametwaliwa kwa muda mrefu na wawekezaji waweze kulipwa fidia yao na waweze kutimiza kupata haki yao ya kukaa katika maeneo hayo?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Waitara, Mbunge wa Tarime Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sera yetu, sheria za ardhi pamoja na uwekezaji nchini ziko wazi. Kwamba pale inapotokea mwekezaji yeyote anahitaji kutumia ardhi, ardhi ambayo ina mmiliki halali na shughuliki yake anaifanya, labda kwa kilimo, alijenga nyumba za makazi au uwekezaji kama ulivyosema, pindi ardhi hii inapotakiwa; iwe na Serikali au mwekezaji ni lazima apate fidia.

Mheshimiwa Spika, utaratibu unaotumika, baada ya kuwa mwekezaji ameomba kulitumia eneo hilo, uthamini utafanywa na mthamini wa Serikali, gharama zitapatikana na mhusika wa ile ardhi atahusishwa. Thamani ile ikishapatikana, kama ni Serikali, Serikali italipa, na kama ni mwekezaji atapewa ile gharama ya ule uthamini uliofanywa na atapaswa kulipa.

Mheshimiwa Spika, umetamka maeneo mengi, na mimi nimepata nafasi ya kupita maeneo kadhaa, tumekuta baadhi ya Watanzania waliokuwa wanamiliki ardhi kihalali wametoa ardhi yao kwa shughuli hizo za uwekezaji. Iwe ni kwenye madini au kwa shughuli nyingine yoyote ile ili mradi ni uwekezaji hawa wote wanapaswa kulipwa. Na nitoe wito kwa Wizara ya Ardhi ambayo ndiyo inasimamia sheria, kuhakikisha kwamba Watanzania ambao wanachukuliwa ardhi yao waliyomilikishwa kihalali, ni lazima walipwe fidia ya ardhi yao ili haki iweze kutendeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ni muhimu sasa pia hata kwa mamlaka za Serikali za Mitaa pale ambako wananchi wapo wamechukuliwa ardhi yao kwa uwekezaji, kwa shughuli nyingine yoyote ile na wanahitaji kulipwa fidia, ni lazima haki yao waipate kwa kulipwa fedha hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba inapotekea kuna madai kama bado madai yatolewe. Na hasa kama kumefanyiwa uthamini basi ile thamani ya ile ardhi au thamani ya ile mali iliyochukuliwa kwa ajili ya kupisha kwa shughuli nyingine ni lazima iweze kulipwa. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister