Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 31 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2022-05-26

Name

Assa Nelson Makanika

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Kaskazini

Primary Question

MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu inapitia katika wakati mgumu wa kuagiza mafuta ya kula nchi nyingine. Zaidi ya nakisi 250,000 mpaka 300,000 za mafuta ya kula zinaagizwa nchi zingine ambapo tunatumia zaidi bilioni 480 kuagiza nakisi hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika kupunguza uagizwaji wa mafuta ya kula, bonde la Tanganyika, kwa maana ya Mikoa ya Rukwa, Kigoma na Katavi, ina ardhi nzuri sana ambayo ikitumiwa vizuri inaweza ikasaidia nchi katika kupunguza nakisi hii. Je, ni nini mkakati wa Serikali katika kuwakaribisha wawekezaji wakubwa ili kuweze kusaidia kupunguza nakisi ya kuagiza mafuta hayo nchini?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Makanika, Mbunge wa Kigoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Makanika ni shahidi wa jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali sasa za kuhamasisha kilimo cha michikichi ambacho pia kinatoa mazao haya ambayo pia yanakamua mafuta kwa lengo kudhibiti nakisi hiyo tuliyonayo ya upungufu wa mafuta hapa nchini, au kupunguza kiwango cha uagizaji mafuta kutoka nje. Tayari zoezi hilo tumelisimamia vizuri na mimi mwenyewe nimekwenda Kigoma mara kadhaa, nimehamasisha kilimo, tumeanzisha kituo cha utafiti, tumezalisha na mbegu na tumesambaza kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, na sasa tumeanza kupata matumaini. Nimekwenda kwa mara ya mwisho nimekuta michikichi inaanza kuiva, kwa hiyo, tayari sasa kwa jitihada hizi. Lakini chikichi haistawi tu pale Mkoani Kigoma, pamoja na mikoa hiyo ya Katavi na Mpanda lakini na miko yote ambayo inalima zao la nazi inaweza pia kustawisha zao la chikichi.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kuwahamasisha wakulima waliopo maeneo hayo yanayolimwa minazi walime pia na michikichi. Tunaamini kampeni hii ambayo tunaendelea nayo ambayo pia Watanzania wanaopenda kilimo wakiendelea kupanda michikichi tutapunguza nakisi lakini pia tutaokoa na fedha tunazozitumia kuagiza mafuta nje. Sasa nini kinafanyika sasa, kwanza tunahamasisha wakulima wadogo wadogo wenye uwezeo wa kulima eka moja, mbili mpaka kumi, mia. Tunatoa wito kwa wawekezaji wa ndani na wa nje kuja kuwekeza nchini Tanzania. Tuna ardhi ya kutosha, hata kule Kigoma tuna ardhi ya kutosha Mpanda tuna ardhi ya kutosha, Katavi tuna ardhi ya kutosha, Sumbawanga nako pia tuna ardhi ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunatoa wito kwa wawekezaji kuja nchini Tanzania kuwekeza kwenye kilimo cha michikichi ili tuweze kuzalisha kwa wingi, tukamue na tuweze kupata mafuta yetu sisi wenyewe, na tunaamini gharama itakuwa ndogo na zile fedha ambazo tunapeleka nje kuagiza mafuta hazitakwenda tena na badala yake zitaingia kwenye mzunguko wa uboreshaji wa miradi ya utoaji huduma hapa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba kampeni ile inayoendelea Kigoma bado inaendelea kwa kutoa wito kwa wawekezaji. Ardhi tunayo, na wakuu wa mikoa na wakurugenzi wamepata taarifa; watenge ardhi kwa ajili ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa tunaenda kwenye viwanda vya ukamuaji. Kwamba, badala ya ile teknolojia ya kushika miti wanazunguka hivi, ambayo nimeishuhudia kule Kigoma, nataka tubadilishe iwe mashine ili iweze kukamua kwa asilimia angalau 99 ya ukamuaji, badala ya ukamuaji wa sasa wa asilimia 70. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe wito kwa Watanzania kujitokeza kulima. Mara kadhaa nimesema, kama unataka kuwekeza kwa ajili ya manufaa ya mtoto wako ambaye yuko shule leo lima mchikichi, mpe shamba la mchikichi, mtoto huyo anapomaliza darasa la saba tayari ana shamba lake la eka mbili, tatu, nne, anapokwenda kidato cha kwanza mpaka cha nne anakuta shamba lake lipo, hata anapokwenda chuo kikuu anakuta shamba lake lipo na anaanza kuvuna yeye mwenyewe, na linavunwa lile zaidi ya miaka 30. Kwa hiyo, ni uwekezaji mzuri mkubwa na niendelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister