Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 31 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2022-05-26

Name

Oran Manase Njeza

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa kuna miradi mingi ya miundombinu inayosubiri kutekelezwa kwa bajeti ya Serikali na bajeti ya Serikali; na bajeti ya Serikali imekuwa inatengwa kwa kutumia fedha za ndani na fedha za nje, lakini mfumo huu umeonesha kuchelewesha miradi na hata kupelekea gharama ya miradi kuwa kubwa:-

Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kuanza kutumia mfumo wa PPP au mfumo wa EPC plus finance ambao ni mfumo wa Engineering, Procurement na Construction ambao umeonesha mafanikio makubwa sana kwa nchi za Afrika Mashariki na hata SADC ili kupunguza gharama za utekelezaji? Ahsante sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara zake, tunaleta bajeti zetu hapa na Waheshimiwa Wabunge mnapitisha bajeti hizi. Siwezi kusema kwamba bajeti hizo hazitoshi, lakini najua mahitaji ni makubwa, ni kweli tunahitaji fedha nyingi; na baadhi ya miradi tunapoitekeleza mwishoni mwa mwaka, mingine tunakuwa hatuikamilishi kwa sababu ya mwenendo wa makusanyo ambayo tulikuwa tunategemea kukusanya, kiwango hicho cha fedha ambacho tulikiomba hapa Bungeni, kinaweza pia kisitoshe.

Mheshimiwa Spika, iko mifumo mingine ambayo inawezesha pia kukamilisha bajeti zetu tunapopata fedha kutoka nje ya bajeti inayotegemea mapato ya ndani, kwa sababu bajeti zetu zinategemea mapato ya ndani, na pia tuna marafiki zetu wanaongeza mtaji na tunatekeleza majukumu yetu. Hii ndiyo tunafanya kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, sasa tunapokwenda kukusanya na tusifikie malengo, tunatafuta njia nyingine ikiwemo na hiyo ya PPP ambayo kwa muda mrefu tumeitekeleza, lakini imekuwa ngumu kidogo kutekeleza na tumebadilisha na sheria. Leo Mheshimiwa Njeza amependekeza mfumo wa EPC plus finance, najua Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi ameizungumzia sana mfumo huo juzi hapa wakati wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu unatafuta mwekezaji ambaye atakuwa tayari kutekeleza mradi wa aina fulani, anautengenezea mchoro wake, tunakaa naye, tunakubaliana naye, tunampa kazi hiyo ya manunuzi, ujenzi; na tunapokwenda kujenga, gharama ya mradi anaitumia yeye, na sisi tunaupokea mradi kwa yeye kuujenga, halafu kuufanyia kazi na wakati mwingine anaweza kuurudisha kwetu tuutumie baada ya kuwa ametumia kwa kipindi fulani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, miundombinu ile inabaki kwetu sisi. BOT (Build, Operate and Transfer System), hiyo inaweza kuwa inaendelea kutumika kwa utaratibu huo. Kwa hiyo, mfumo huo tunaukubali Mheshimiwa Njeza, ushauri wako nakuahidi tunauchukua, ni mfumo mzuri na Waziri wa Ujenzi yupo, Wizara ipo, itatumia mfumo huo na Wizara ya Fedha ipo, itaangalia mwenendo wa mapato yetu, nao ndio wanaoweza kuangalia mfumo huo tunaweza kupata kwa kiasi gani; na kama tunakopeshwa gharama yake ni kiasi gani? Kwa maana hiyo, tutakubali mfumo huo pale ambako tunaweza kupata mkopo huo wenye gharama nafuu ili tuweze kutekeleza miradi yetu.

Mheshimiwa Spika, nataka nimwakikishie Mbunge na Waheshimiwa Wabunge kwamba ile miradi yetu tuliyoipendekeza kuitekeleza kwenye bajeti hii, hata kama hatutakusanya kwa kiwango cha kutosha, mapato ambayo tunayo, tutatumia mfumo ambao Mheshimiwa Njeza ametupendekezea hapa kwa sasa, ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister