Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 31 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2022-05-26

Name

Priscus Jacob Tarimo

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kumwuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, urasimishaji wa makazi yaliyojengwa holela kwenye miji mingi katika nchi yetu ni zoezi ambalo lina gharama kubwa lakini mwisho wake yale makazi hayawi na ubora unaotakiwa hata kufikika na hata kwenye anuani za makazi yana shida kwa sababu barabara na huduma nyingine haziko vizuri:-

Mheshimiwa Spika, ni nini mpango wa Serikali wa kupima maeneo katika maeneo ya Miji, Manispaa pamoja na Majiji na yale maeneo ya pembezoni ili kuhakikisha sasa tunaipanga miji yetu vizuri na huduma zinawafikia wananchi? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia suala la upimaji wa ardhi kwenye maeneo yetu ikiwemo na maeneo ya miji ambayo yeye ameeleza. Nataka nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango huu ni endelevu ndani ya Wizara yetu ya Ardhi, kuhakikisha kwamba tunapima maeneo yote ya ardhi nchini na kwenye vipimo hivi tunabainisha huduma zote zinazotakiwa kutumika kwenye ardhi hiyo; kwanza makazi, maeneo ya taasisi, maeneo ya huduma za jamii kama vituo vya mabasi na masoko na kila kitu. Huo ndiyo mkakati ambao sasa unaendelea chini ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kinafanyika baada ya kuwa tumekamilisha kupima, tunakabidhi kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa ambapo wao ndiyo wanaitunza ile ardhi na kuitumia na kuitoa kwa Watanzania ambao wako kwenye maeneo hayo. Pia hata kwenye mamlaka yenyewe inaweza kuwa inapanga sasa mipango yake. Kwa mfano, pale Moshi Mjini, baada ya kuwa tumeupima ule mji na kupanga matumizi yake, tunawakabishi Manispaa ya Moshi ili waanze kupanga sasa, hapa panatakiwa masoko, hapa vituo vya mabasi, maeneo mengine makazi na kila kitu. Kwa hiyo, mkakati huu ni endelevu na siyo tu kwa maeneo ya miji, tunakwenda sasa mpaka vijijini.

Mheshimiwa Spika, tunataka Watanzania sasa wapate maeneo yaliyopimwa, yanayotambulika rasmi ili pia tuweze kuwapa hati. Ile hati inawasaidia pia kama mtaji wa kukopea kwenye mabenki na taasisi nyingine za fedha. Kwa hiyo, malengo yetu ni endelevu na ni mapana kidogo kwa sababu tunataka kila Mtanzania anufaike na ardhi iliyoko nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naitaka sasa Wizara ya Ardhi kuendelea kukamilisha zoezi hili ili Watanzania wanufaike na ardhi waliyonayo kwenye maeneo yao. Kwa kufanya hivyo, itawezesha pia hata wawekezaji kujua wanapofika wanaambiwa eneo la uwekezaji lile pale, litakuwa limeshapangwa tayari. Kwa hiyo, mnakamilisha kwa kushirikiana na Mamlaka za Serikali za Mitaa ambapo pia kuna Afisa wetu wa Ardhi. Hhii sera ni endelevu na itakuwa na msaada mkubwa kwa Watanzania, ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister