Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 8 Lands, Housing and Human Settlement Development Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2024-02-08

Name

Salim Mussa Omar

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Gando

Primary Question

MHE. SALIM MUSSA OMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa letu linapitia katika changamoto kubwa ya migogoro ya ardhi sasa hivi, jambo ambalo linakuwa linazorotesha sana shughuli za kimaendeleo katika nchi yetu. Wananchi walio wengi wamekosa imani na Watendaji wa Wizara ya Ardhi. Je, hatuoni sasa kama ni muda muafaka wa kuweza kupitia mifumo ya utendaji katika Wizara hii ili kuweza kuepukana na changamoto hii? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salim Omar, Mbunge wa Gando Zanzibar, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninakiri kwamba tuna migogoro mingi ya ardhi nchini na migogoro hii inatokana na mahitaji makubwa sasa ya matumizi ya ardhi hiyo, iko migogoro ya wakulima na maeneo yaliyohifadhiwa, iko migogoro ya wafugaji na maeneo yaliyohifadhiwa, lakini tuna migogoro hiyo iliyosababisha na utoaji wa hati mbili mbili kwa kiwanja kimoja na mipaka. Sasa nini Serikali inafanya? Kwa sasa hivi tunaendelea na maboresho ya Sera yetu ya ardhi nchini. Tunaamini Sera hii ikikamilika kuandaliwa ikipitishwa hapa kwetu Bungeni itasaidia sana kupunguza matatizo ya ardhi, kwa sababu kwenye Sera tutaainisha maeneo yale ambayo tumepata uzoefu wa migogoro yake kwa wakati huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kukabiliana na changamoto hii wakati huu tunaendelea kuiandaa sera, Serikali imeendelea kufanya maboresho ya utoaji vibali vya ardhi kwa wakulima na wale wanaotaka kujenga miundombinu mbalimbali. Mifumo hii tunaendelea kuihimarisha mifumo ya ki-electronic ili ipunguze kitendo cha kutumia makaratasi pekee katika utoaji wa vibali vya matumizi ya ardhi. Tunajua pia kwamba kuna Watumishi wachache kwenye Halmashauri zetu na Wizara ya Ardhi wanaokiuka taratibu na sheria tulizonazo kwenye ardhi na utoaji vibali kwa watumiaji wa ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine hulazimika kutoa Hati Mbili kwenye kiwanja kimoja hapo lazima mgogoro utakuwepo, ikiwemo na kuimarisha sheria tulizonazo maeneo yale yenye migogoro. Kwa hiyo Serikali kazi kubwa tunayoifanya sasa ni kutoa elimu na elimu hii tunashirikisha wananchi waweze kujua Sheria zetu za Ardhi na matumizi yake lakini pale ambako tunaona tunahitaji kufanya maboresho, Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya wanaendelea kwenye maeneo yao kusikiliza kero mbalimbali kwa wananchi ili kutatua migogoro ya ardhi pale ambako kero hiyo inawasilishwa kwa Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaendelea kutoa wito kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kote nchini kuendesha vikao vinavyokusanya wananchi wenye changamoto na kusikiliza changamoto zao ikiwemo na ardhi, ili kutatua changamoto hizi na wananchi waweze kufanya shughuli zao kikamilifu. Tunaahidi kwamba migogoro hii tutaipunguza kwa kiasi kikubwa, kwa sababu sera ambayo inaandaliwa na utekelezaji wa kufuata sheria na usikilizaji wa kero kwa wananchi utasaidia na hasa matumizi ya ki-electronic ambayo tunaendelea sasa kuyaboresha ndiyo ambayo yataendelea kupunguza kero za ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ni kwamba sasa hivi tumesogeza huduma za ardhi mpaka kwenye ngazi ya Mikoa. Mikoa yote tumepeleka Makamishna wa Ardhi ambao watasaidiana, watashirikiana na Mkuu Mkoa kutatua matatizo na Halmashauri zilizoko ndani ya Mkoa, lakini mpango wa baadaye pia ni kushusha Mamlaka za Ardhi ambazo zitakwenda kutatua matatizo hayo hasa kwenye maeneo ya Majiji na Manispaa ambayo kuna idadi kubwa ya watu na mahitaji makubwa ya viwanja ili huduma hii iweze kupatikana huko huko kwa ukaribu zaidi. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister