Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 8 Community Development, Gender and Children Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2024-02-08

Name

Nusrat Shaaban Hanje

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na maendeleo makubwa ya kiteknolojia duniani, watoto wetu wamekuwa wakiingia kwenye mitandao na wakitumia vifaa vya ki-electronic kwa ajili ya kujifunza masuala ya TEHAMA na masuala mengine ya kujipa maarifa katika masomo yao. Tunafahamu wanapoingia katika mitandao wanakutana na mambo mengi ambayo yanaweza kupelekea mmomonyoko wa maadili na udhalilishaji wa watoto mitandaoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu mwaka 2014 Umoja wa Mataifa ulielekeza dunia kuweka mikakati madhubuti ya kuwalinda watoto dhidi ya ukatilii wa mitandao. Nchi nyingi zime-adopt, zimeweka sera madhubuti na sheria madhubuti za ulinzi wa watoto mitandaoni. Sasa nchi yetu imekuwa ikiendesha kampeni zisizo rasmi za ulinzi wa watoto mitandaoni, naomba kufahamu Serikali imejipangaje kuhakikisha inatengeneza mazingira bora ya kisera na ya kisheria kuhakikisha kwamba online child protection inapewa nguvu. Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, dunia sasa hivi inaendea kwenye maendeleo makubwa ya matumizi ya mifumo yetu mbalimbali ki-electronic. Pia dunia imeanza kuelimisha umma wake kutumia mifumo hii ya ki-electronic kwa urahisi zaidi, sasa mifumo hii imekuja ikiwa na faida lakini pia kuna changamoto zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zilizopo ni miongoni mwa hayo uliyoyaeleza kwamba jamii baadhi yetu tunatumia vibaya matumizi ya TEHAMA, matumizi ya Mifumo hii ya ki-electronic vibaya kwa kukashfu, kutumia mitandao kudhalilisha watu wakiwemo watoto na wanawake, lakini pia hata juzi tulipokuwa tunapitisha Muswada wetu hapa wa Vyama vya Siasa tulilizungumza hili na tumeliwekea mbano kidogo wale ambao watatumia vibaya mitandao kwa ajili ya kudhalilisha kwenye eneo la siasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa huu ni mkakati ambao Serikali pia tumekubaliana na tumesaini mikataba ya kimataifa kukabiliana na unyanyasaji, vitendo vya kikatili kwa watoto na wanawake. Sisi kama Serikali tumeweka utaratibu wetu kupitia Wizara yetu ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto ili kukabiliana na wale wote wanaotumia vibaya mifumo hii kwa kudhalilisha watoto, wanawake na makundi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu ambao tumeufanya huku tukiwa tunapeleka pia kwenye Mtaala wetu wa elimu kufundisha kutoka Shule za Msingi, Sekondari, Vyuo mbalimbali mpaka elimu ya juu, elimu hii ya matumizi ya ki-electronic tumeweka pia na Sheria zinazowabana hawa wote wanaotumia vibaya mitandao hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali inaendelea kuwahakikishia Watanzania kwamba, tutaendelea kuimarisha kudhibiti wale wote ambao wanatumia vibaya mitandao hii na tutachukua hatua kali dhidi ya wale wote ambao watatumia vibaya matumizi haya ya TEHEMA kwa kudhalilisha na kukatili wengine wa aina yeyote ile kwao ili itoe mafundisho kwa wengine ambao wanaweza kuungana nao kwenye matumizi mabaya haya. Kwa hiyo, nitaendelea kuwahakikishia ya kwamba matumizi ya TEHAMA tutaendelea kuhamasisha yake lakini hamasa hii ni kwa matumizi sahihi na siyo vingine. ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister