Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 8 Finance and Planning Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2024-02-08

Name

Ng'wasi Damas Kamani

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kwa kupata nafasi kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Natambua kwamba mwaka 2006 Bunge hili lilipitisha Sheria ya Benki ya Tanzania, ambayo chini ya kifungu cha 27(1)(b) inaipa Mamlaka Benki hii ku-design fedha kwa kuweka nembo na material mbalimbali. Pia natambua mwaka 2021 nchi hii imepata Rais wake wa kwanza Mwanamke anaefanya kazi nzuri na anatambulika katika Bara la Afrika na Duniani kama Rais madhubuti na wa mfano. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri Mkuu, natambua pia kwamba Bunge la Marekani sasa lipo katika utaratibu kupitisha sheria ambayo itawezesha Harriet Tabman, mwanamama, mwanaharakati aliyefanya kazi kubwa kwenye vita dhidi ya utumwa, kuwekwa kwenye dola ishirini kama kumbukumbu. Natambua kwamba katika Bara letu la Afrika nchi kama Nigeria, Malawi na Tunisia zimekwishafanya hatua hizi na zimetambuliwa na Benki ya Dunia na IMF kama hii hatua katika uelekeo unaofaa. Je, Serikali haioni sasa kwamba kuna haja ya kuweka kumbukumbu ya kudumu kwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka picha yake katika fedha za nchi hii? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’wasi, Mbunge Vijana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameonesha kutambua kazi nzuri, mchango unaotolewa na Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuona kama je, Serikali inaweza kuona umuhimu wa kutumia picha yake kwenye fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uwekekaji wa picha za viongozi mbalimbali ni maamuzi ambayo huko nyuma tulitoa kwa lengo la kukumbuka mchango wa Viongozi hawa kwenye Taifa hili, hasa picha ambazo zinatumika sasa za Baba wa Taifa hili, Mwalimu Julius Nyerere lakini pia na Mheshimiwa Sheikh Abeid Aman Karume Rais wa kwanza wa Zanzibar ili kutambua tu mchango wao walioutoa katika Taifa hili na kwa hiyo picha zao zilitumika kama sehemu ya kumbukumbu zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunazo aina ya fedha noti na hizi sarafu ambazo pia tunatumia kuweka alama za wanyama wetu. Hii ilikuwa ni kuenzi tunu ya Taifa lakini pia kuuboresha hamasa kwenye Utalii. Sasa maamuzi ya kuweka picha kwenye noti mara nyingi yanafanywa na maamuzi ya kiongozi mwenyewe kwa kushauriana na Benki Kuu. Sasa kwa kuwa umelileta hili na sisi tunatambua kuwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa mchango mkubwa kwenye Taifa hili, niseme tu tunapokea ushauri wako na litaingia Serikali litajadiliwa, pale ambako watafanya maamuzi kwa kushauriana na Benki Kuu taarifa zitatolewa rasmi. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister