Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 8 Industries and Trade Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2024-02-08

Name

Cecil David Mwambe

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Primary Question

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru pia kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imefanya juhudi kubwa sana kwa kipindi kirefu kuondoa tozo mbalimbali hasa zaidi kwenye mazao ya biashara kama vile pamba, kahawa, korosho pamoja na mazao mengine. Nia ya kuondoa tozo hizi ilikuwa ni kumletea nafuu mnunuzi ambaye naye anakwenda kumpelekea nafuu mkulima ili aweze kupata faida nzuri kwenye mazao yake ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo siku za karibuni kumeonekana kama tozo zilikuwa zinajirudia na kusababisha kuanguka kwa bei ya mazao ya kilimo, ikiwemo ya Korosho. Ni nini, kauli ya Serikali kuhusu kufanya marejeo ya tozo mbalimbali ambazo zinaathiri bei ya Korosho? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba haya mazao yetu yote na hasa yale mazao yanayolimwa kwa ushirika kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameyataja, ni mazao ambayo miaka mingi huko nyuma kumekuwa na ongezeko la tozo mbalimbali na ikasababisha hata kuanguka kwa bei na pia kero kwa wakulima kwa kupata kipato kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulifanya mapitio kwenye mazao yote yenye bodi na yanayouzwa kwa mifumo ya ushirika na kugundua kwamba tuna makato mengi. Mazao mengine yana makato mpaka 30 au 20. Tulifanya hizo jitihada kupunguza makato hayo na kufikia kiwango cha mwisho makato sita na kuleta unafuu mkubwa kwa wanunuzi na pia kuwapa kipato cha kutosha wakulima. Hiyo inaendelea hata sasa, mazao aliyoyataja pamoja na kakao kule Kyela, sasa hivi bei imepanda juu sana baada ya kuwa tumesimamia kuondoa tozo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali bado inaendelea na imeshatoa maagizo kwa bodi zote za mazao kufanya mapitio ya mara kwa mara ya tozo na pia mwenendo wa soko la mazao yenyewe. Lengo hapa, tunataka Serikali tuone kuwa mkulima anayelima zao hili, ambaye anatumia muda wake mwingi kulima zao hili, ananufaika kwa kupata bei nzuri. Sasa, bei nzuri ni pale ambapo tunapunguza gharama kwa wanunuzi ili gharama hiyo iweze kuhamia kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato huu unaendelea na hasa usimamizi wa Vyama hivi vya Ushirika vya Msingi ambako ndiyo kunaanza kuwekwa kwa tozo, pia vyama vyake vikuu ambako nao ndio wanatoa vibali vya tozo kuhakikisha kwamba tozo hizi haziendelei. Tumeweka ukomo wa tozo muhimu kwenye zao husika kulingana na mazingira waliyonayo ili kuweza kuleta unafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie kuwa Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote ambao mnatoka kwenye maeneo yanayolima mazao yenye bodi na kuuzwa kwa ushirika kwamba, Serikali itaendelea kusimamia kwa ukaribu, kuhakikisha kwamba wakulima wananufaika na mazao haya kwa kuwatafutia masoko, lakini baada ya kuwa tumeuza tozo mbalimbali zisiingie bila kuwa na utaratibu. Bodi nazo tumesisitiza kufanya ufuatiliaji wa kuhakikisha kwamba hakuna tozo nyingi kwenye eneo hili ili makundi haya mawili; wanunuzi na wakulima waweze kunufaika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister