Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 14 Natural hazards and Disasters Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2024-04-25

Name

Cosato David Chumi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na napenda pia kutumia nafasi hii kupongeza jitihada za Serikali katika masuala mazima ya hali ya hewa. Kwa kweli taarifa zinazotolewa zimekuwa na usahihi wa hali ya juu na zinatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nchi yetu pamoja na ushiriki wa uhifadhi na mazingira, lakini pia Mheshimiwa Rais wetu amekuwa mshiriki wa Mikutano ya Kimataifa ya Mazingira. Mara zote ameyasihi mataifa makubwa ambayo kwa kiasi kikubwa yana mchango mkubwa katika mabadiliko ya tabianchi, kutoa fedha kwa ajili ya kusaidia nchi hizi ambazo zinaendelea ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama sehemu ya ushawishi wake, mataifa makubwa kupitia Umoja wa Mataifa walikubaliana kuanzisha Mfuko wa Fidia unaitwa Loss and Damage Fund, kwa ajili ya kuzisaidia nchi zinazoendelea pale ambapo zinakuwa zimepata athari kama hizi zinazoendelea za mafuriko kama matokeo ya tabianchi. Je, Serikali iko tayari kuunda kikosi kazi ambacho kitahusisha wataalam kutoka vyuo vya elimu ya juu, sekta binafsi na NGOs na wataalamu kutoka Serikalini ili kuona kwa namna gani sisi tunapata fedha hizo ili ziweze kutusaidia kukabiliana na athari ambazo zimetokana na mabadiliko haya ya tabianchi?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chumi, Mbunge wa Mufindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali yetu imekuwa inashiriki mikutano mingi na pia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshiriki mikutano mingi, pia Makamu wa Rais Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango ambaye ndiye mwenye ofisi yenye dhamana ya mazingira ameshiriki mikutano hii. Serikali tumeihakikishia dunia kwamba na sisi tuko kwenye mchakato na mpango unaoweza kudhibiti uharibifu wa mazingira hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kuunda chombo, tayari Wizara ya Mazingira ndani ya Ofisi ya Makamu wa Rais inayo timu ambayo inafanya kazi wakati wote pamoja na Idara ya Mazingira kuhakikisha kuwa inakuwa na mipango ya sasa endelevu ambayo itawezesha Serikali yetu kutambua na kubaini maeneo ambayo yanahitaji kuimarishwa kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira. Pia tathmini na tafiti mbalimbali zimekuwa zinafanyika ili ziweze kutuongoza Serikali katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mpango huu unaoendelea ndani ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira ni endelevu kwa sababu tunahitaji kuelimisha umma na tunaona ghasia za mabadiliko ya tabianchi zinazojitokeza kwenye maeneo yao. Lengo hapa ni kupitia tafiti hizo zinazofanywa na kikosi kazi hicho ambacho tayari kimeshaundwa, tutaona mahitaji zaidi ili tuongeze vikosi kazi kulingana na mahitaji yenyewe. Lengo ni kufikia hatua nzuri ili Taifa letu tuwe kwanye nafasi ya kuhifadhi mazingira na kuepusha majanga yanayoweza kujitokeza. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister