Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 42 Industries and Trade Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2024-06-06

Name

Lucy Thomas Mayenga

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Wakuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kutokana na nchi yetu uchumi kuboreka na kuendelea kukua na hali ya amani iliyopo katika Taifa letu, kumekuwa na ongezeko kubwa sana la wafanyabiashara wa ndani ya nchi, lakini vilevile wawekezaji na wafanyabiashara kutoka nje kitendo ambacho kimekuwa kikipanua na kuendelea kuweka wigo mpana zaidi kwenye ufanyaji wa biashara.

Mheshimiwa Spika, lakini kumekuwa kuna tatizo kwamba baadhi ya wafanyabiashara na wawekezaji ambao wanakuja kufanya biashara hapa Tanzania wamekuwa wakifungua biashara au wakifungua viwanda, lakini wamekuwa wanakwenda kwenye ngazi ya chini kabisa kule vijijini kitu ambacho kinasababisha wale Watanzania ambao ni wafanyabiashara au watanzania wananchi wa kawaida kushindwa kufaidika na biashara hizi katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kujua, je ni lini Serikali italeta sera nzuri ili kuweza kumnufaisha Mtanzania huyu walau baadhi ya wafanyabiashara wafikie kwenye level fulani waishie huko kwenye uzalishaji na huku kwenye usambazaji na kufungua maduka mengine mpaka ngazi za chini kazi hizi zifanywe na Watanzania kama ilivyo kwenye baadhi ya nchi za wenzetu? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Mayenga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nitambue mchango wa wafanyabiashara wadogo ambao wananchangia sana kwenye pato letu la Taifa kutokana na shughuli zao za kibiashara, wanalipa kodi na tunaendelea kutunisha mfuko wetu. Pia nchi yetu inayo sera ya mahusiano ya kidiplomasia na nchi marafiki ambao pia wamefungua milango kuingia nchini kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo biashara.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu pia inazo sheria na kanuni ambazo zinaongoza wageni hawa kufanya shughuli mbalimbali hapa nchini ikiwemo biashara, lakini kwa vibali maalumu ambavyo pia vinazingatia aina ya biashara ili kuruhusu Watanzania kufanya biashara nyingi huku ndani.

Mheshimiwa Spika, kutokana na mwingiliano wa wengine kuacha biashara ya ngazi yao kulingana na vibali vyao na kufanya biashara ambazo Watanzania wangeweza kufanya, Serikali tumeimarisha ufuatiliaji wa vibali hivi ambavyo tumevitoa kwa hawa wageni ambao wanafanya biashara ili kuzuia kuingia kufanya biashara ambazo ni fursa kwa Watanzania ili waweze kujipatia mapato yao.

Kwa hiyo, taasisi ambayo inatoa vibali vya kazi inazingatia sana vibali wanavyovitoa ili kuzuia mianya ya wageni kuja kufanya biashara za wananchi wa Tanzania ikiwemo biashara ndogo ndogo.

Mheshimiwa Spika, hili ndilo ambalo Serikali yetu imeweka mazingira ya wafanyabiashara wadogo kufanya biashara zao kwenye maeneo maalumu kama vile hapa Dodoma eneo la Machinga Complex, lakini maeneo mengine yote tulitoa kibali cha halmashauri kuandaa maeneo ya wafanyabiashara wadogo ili isaidie hata ukaguzi na ufuatiliaji tunaoufanya wa kukuta wageni ambao hawakupata vibali vya kufanya biashara hiyo, wanafanya biashara hiyo na huwa tunaendelea kuzuia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania na wafanyabiashara kwamba sera tunayo ya kuwawezesha wafanyabiashara kufanya biashara zao kwenye ngazi za chini bila kuingiliwa na watu wa mataifa ya nje na ufuatiliaji huu unabaini haya yote na tunaendelea kuusimamia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa miongozo aliyoitoa kwa ajili ya kuimarisha biashara ndogo nchini na kutengeneza mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara wetu kufanya biashara kwa uhuru mkubwa kwa ajili ya kupata kipato chao, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister