Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2020-2025 | Session 18 | Sitting 8 | Youth, Disabled, Labor and Employment | Maswali kwa Waziri Mkuu | 3 | 2025-02-06 |
Name
Asia Abdulkarim Halamga
Gender
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumekuwa na ongezeko kubwa sana la vijana nchini wenye uwezo wa kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi kupitia fani mbalimbali katika halmashauri zetu, kutokana na uimara wa sera. Je, ni upi mpango wa Serikali kutambua vijana hawa katika halmashauri zote nchini?
Name
Kassim Majaliwa Majaliwa
Gender
Male
Party
CCM
Constituent
Ruangwa
Answer
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Asia Halamga, Mbunge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli vijana wetu sasa ndio nguvu kazi yetu. Wako vijana wabunifu na wana ujuzi, lakini wapo ambao bado hawajapata ujuzi. Serikali yetu imeandaa mkakati wa kuwawezesha vijana kitaaluma. Kupitia mpango huu, Serikali kupitia Sera yetu ya Vijana na Uwezeshaji imesisitiza na kuhamasisha vijana kushiriki katika shughuli ambazo zinaweza kuleta ujuzi, pia tumehamasisha ubunifu kwenye maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ina mpango ambao sasa unatekelezwa mpaka kwenye halmashauri zetu, kuhakikisha kwamba vijana wenye ujuzi, lakini ambao hawana ujuzi kupata ujuzi. Serikali tumeendelea kujenga Vyuo vya Ufundi, ambavyo vitakuwa vinafundisha masomo mengi ili kuwapa ujuzi vijana wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wako ambao hawajasoma, lakini ni wabunifu wameweza kubuni kazi zao. Wizara ya Elimu imebuni mfumo wa kuitisha pamoja wabunifu na kuandaa maonesho ya ubunifu, ambapo vijana na Mtanzania yoyote atapata nafasi ya kwenda kuonesha kazi yake. Hawa vijana wote wanatoka kwenye halmashauri na katika halmashauri ndiko ambako tumejenga VETA zetu ili kutoa nafasi ya karibu kwa vijana hawa kwenda kujifunza na kupata ujuzi.
Mheshimiwa Spika, ambacho kinafanywa sasa kama ambavyo Mheshimiwa Asia ametaka ni kwamba, halmashauri baada ya kuwa wamepata wabunifu inawabeba kuwapeleka kuonesha ubunifu kwenye maonesho mbalimbali. Baada ya maonesho yale, hawa wabunifu wanatambuliwa, wanawezeshwa aina ya utambuzi wao ili waweze kuendeleza ubunifu wao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutaendelea kuziagiza halmashauri, kuendelea kusimamia ufundishaji wa taaluma zenye ujuzi ili kupata vijana wengi ambao watapata taaluma za ujuzi, pamoja na wale wabunifu ambao mtu mmoja mmoja anaweza kubuni kazi yake waziendeleze, halafu waratibiwe na kutambulika. Tutajua huyu mjuzi yuko wapi, amefanya kazi gani, aina gani na kumtafutia hata uwezekano wa kuwa na masoko pindi ubunifu huo au ujuzi huo unaweza kumuingiza kwenye masoko na maeneo mengine ya ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, halmashauri zetu ziendelee kuratibu vijana hawa kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamiii ambayo tunayo katika kila halmashauri, tuweze kuwatambua. Wale ambao wanafanya kazi ya aina moja waundiwe vikundi ili wawezeshwe kupata hata mitaji kupitia mikopo ya halmashauri au mifuko yote au Taasisi za Fedha, waweze kuendeleza ujuzi huu.
Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba, vijana hawa tunawaweka pamoja kwenye maeneo hayo. Nawaagiza sasa wahakikishe kwamba, kila halmashauri inakuwa na kanzidata ya kuwatambua hawa vijana ili kuwawezesha kushiriki kwenye maonesho makubwa na kuboresha kazi zao na kuwapa mitaji ya kuendeleza kazi hiyo. Hayo ndio maelezo ya swali hili. Ahsante sana. (Makofi)
Copyright © Bunge Polis 2025. All Rights Reserved