Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 18 Sitting 13 Regional Administration and Local Government Authorities Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2025-02-13

Name

Tarimba Gulam Abbas

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kinondoni

Primary Question

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote ninamuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu apokee salamu kutoka kwa wananchi wa Kinondoni, ukamwambie Mheshimiwa Rais kwamba tunaridhika na tunafurahi kuona kwamba ametuondolea shida za Kinondoni. Hatudaiwi sekondari, hatudaiwi elimu, hatudaiwi afya, ametuletea shilingi trilioni 1.3 kwa ajili ya mradi wa Daraja la Jangwani na vilevile pale Kigogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu mimi Mheshimiwa Waziri Mkuu linahusu barabara za ndani.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, wakati wote tunajua barabara za ndani ni kiungo muhimu sana kwa uchumi wa watu na uchumi wa Taifa hili, zimekuwa na gharama kubwa, Mheshimiwa Rais na Bunge hili limekuwa likizungumzia juu ya umuhimu wa utunzaji wa barabara zile ambazo barabara moja sasa hivi inafikia kwa kilometa moja shilingi bilioni 1.3, lakini ukarabati na utunzaji wake ni wa matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, inafika wakati mashimo hata yakiwa madogo yanaachwa mpaka yanakuwa makubwa kiasi kwamba utengenezaji wake unasubiri utaratibu wa manunuzi ya mkandarasi, huku mashimo yanaongezeka. Hata ikitokea kalvati likivunjika linasubiri mkandarasi binafsi aje kutengeneza. Sasa suala hili linasababisha Serikali iendelee kupata hasara katika utunzaji wa barabara.

Mheshimiwa Waziri Mkuu huoni kwamba mfumo ulioko sasa hivi umefeli, haufanyi kazi? Je, Serikali iko tayari sasa kufikiria kurudisha mfumo uliokuwepo zamani ambapo halmashauri zinatumia karakana zake, mitambo yake midogo kama ilivyo kwenye nchi nyingine kama South Africa ambapo mashimo yakitokea vikosi kazi haraka sana huenda kutengeneza na vinatengeneza kwa ukamilifu kiasi kwamba barabara zile zinakuwa na uhai mrefu wa kuweza kuishi?
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Tarimba, twende kwenye swali.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni hilo nimemuuliza, je, Serikali haioni kwamba inahitaji kubadilisha mfumo wa kutumia wakandarasi binafsi kutengeneza barabara zile, badala yake Serikali irudishe mfumo uliokuwepo awali wa kutumia vikosi kazi vya manispaa au hata TARURA yenyewe wakapewa kazi hizo kuweza kuzifanya badala ya kutegemea mkandarasi binafsi? Nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimba Abbas, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipokee salamu za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya Kinondoni, lakini pia na Taifa zima, salamu hizo zitafika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ukarabati, ujenzi mpya wa barabara nchini tuna uratibu vizuri na tumeufanyia tathmini mara kadhaa. Awali mfumo wa ujenzi wa barabara za vijijini zilikuwa zinakarabatiwa na halmashauri zenyewe, tukagundua kwamba hizi halmashauri zina uwezo tofauti, kuna halmashauri ndogo ambazo hazina uwezo kabisa, kuna halmashauri zenye mapato ya kati, lakini na halmashauri zile zenye uwezo kama Jiji la Dar es Salaam, Kinondoni na maeneo mengine nayo pia yana idara ya ujenzi iliyokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliwasikiliza Waheshimiwa Wabunge wakati wote mlipokuwa mnaomba baadhi ya barabara zenu kwenye halmashauri zihamishiwe TANROADS. TANROADS ni taasisi ambayo tuliiunda kwa kushughulikia barabara kuu na ikaonekana kwamba TANROADS ni wakala ambao unafanya vizuri zaidi. Kutokana na maombi ya mara kwa mara tukaendelea kufanya tathmini ya ukarabati wa barabara za kwenye wilaya, lakini pia na vijijini, ndipo Serikali ilipoamua kuunda wakala mwingine wanaoshughulikia barabara za vijijini ambaye ni TARURA na ndiyo inayosimamia ujenzi wa barabara za kwenye miji na vijijini, na inafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu zaidi ni pale ambapo umesisitiza kwamba ni vizuri kutumia mamlaka yenyewe ikarabati barabara badala ya wakandarasi binafsi. Sasa hili suala linategemea na yule mwombaji aliyeonesha kama ana uwezo, lakini akafanya vibaya. Sasa ambacho tutakifanya kutokana na ushauri wako na ombi lako, tunaendelea kufanya tathmini ya utendaji wa TARURA, lakini hadi sasa TARURA imeendelea kufanya vizuri kwa sababu wameendelea kukarabati, kutengeneza na kujenga barabara, iwe hawajengi wenyewe lakini wanawapa wakandarasi binafsi, wanawasimamia kazi hizo na tunaona mafanikio yanayofanywa na TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata kipindi hiki ambako mvua nyingi zimenyesha nchini na barabara nyingi zimeharibika, TARURA wanaendelea kufanya kazi na sisi tunaongeza bajeti ili kuongeza uwezo wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo basi, tutaendelea kuchukua ushauri wako na kuangalia mwenendo wa utendaji wa TARURA, lakini hasa wakandarasi binafsi. Tutaitaka TARURA isimamie wakandarasi hawa wanapopewa kazi wawe na uwezo wa kujenga barabara za kudumu kwa mujibu wa viwango vilivyopo ili hizi barabara ziweze kutumika kwa muda mrefu. Tutaendelea kuwapa fedha za matengenezo ya muda mfupi mfupi kwa ajili ya kuziba mashimo pale ambapo panatokea shimo badala ya kukaa kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, tukiwa tunaendelea kufuatilia mwenendo wa utendaji wa TARURA na maoni yenu, sasa niiagize TARURA kujikita katika kuhakikisha kwamba wanapotaka kujenga barabara na wanatoa kandarasi, basi mkandarasi huyo awe na uwezo wa kujenga kwa viwango vinavyokubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia panapotokea uharibifu watumie ile fedha ambayo tunawapa ya matengenezo ya muda mfupi ili kuhakikisha kwamba uharibifu huo unazibwa mara moja na barabara ziendelee kutumika. Huo ndiyo mpango ambao tunao ndani ya Serikali, ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister