Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 18 Sitting 13 Regional Administration and Local Government Authorities Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2025-02-13

Name

Saashisha Elinikyo Mafuwe

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Hai

Primary Question

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza ninaipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo inaratibu zoezi la utoaji wa mikopo ya 10% ya mapato yote ya halmashauri ambapo akina mama wanapewa asilimia nne, asilimia nne - vijana na asilimia mbili wanapewa watu wenye ulemavu. Hivi karibuni yamefanyika maboresho ya kanuni na kuruhusu kundi la vijana umri wake kuongezwa kutoka miaka 35 mpaka 45.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kundi la akina baba limeachwa nyuma, Serikali haioni ni wakati sahihi kuruhusu kundi la akina baba na wao linufaike na mikopo hii, kwa sababu kumekuwa na malalamiko makubwa ya akina baba kukosa fursa hii na wao ndiyo wakuu wa kaya, wao ndiyo wakuu wa familia hizi.

Je, Serikali haioni ni wakati sahihi sasa kufanya marekebisho ya kikanuni ili kundi la wanaume (akina baba) na wao wanufaike kwa mikopo hii bila kigezo cha umri? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, upatikanaji wa fursa za mikopo kwenye maeneo mbalimbali zilifanyiwa tathmini, tukagundua kwamba yapo makundi hayana fursa nzuri, yana fursa ndogo sana kupata mikopo hii. Makundi haya ni yale ambayo baadaye tulianzisha mikopo maalumu ile kupitia halmashauri zetu nao ni walemavu, wanawake na vijana. Hili kundi tuliamua kuanzisha mfuko maalumu kwenye halmashauri zetu ili wapate nafasi ya wazi kupata mikopo kwenye haya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa suala la wanaume kupata nafasi. Hao ndio walikuwa wanapata nafasi ya wazi ya kunufaika na hata baada ya kubadilisha umri, bado ninaona wana nafasi kubwa. Wakati huo vijana wakiwa wanafikia umri wa miaka 35, wanaume ambao ni vijana wanapata nafasi ya kukopa wakiwa vijana, lakini baada ya miaka 35 kwa wakati huo walikuwa pia na fursa za kwenda kwenye taasisi za kifedha na ndiyo fursa ambayo tulifanya tathmini tukagundua kwamba wengi wanaopata mikopo kwenye taasisi mbalimbali za kifedha ni wanaume kuliko akina mama baada ya kufanya tathmini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata baada ya kuwa tumebadilisha kigezo cha kijana kutoka miaka 35 mpaka 45, bado kijana huyu huyu sasa tumemuongezea muda na bado akizidi muda wa miaka 45 anakuwa mtu mzima, vilevile anaweza kupata mikopo.

Kwa hiyo, utakuta kundi hili pia bado lina nafasi ya kupata mikopo kwenye taasisi yoyote ya fedha, lakini pia wana nafasi ya kupata mikopo kwenye halmashauri. Kwa hiyo, utaona kabisa kwamba kundi hili lina fursa ile ya awali ya kuingia kwenye taasisi baada ya miaka 45, chini ya miaka 45 anapata kwenye taasisi na vilevile kwenye mikopo ya halmashauri. Kwa hiyo, fursa hii tumeigawa hivyo, tunajua kabisa haya makundi yote yanaweza kupata nafasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni nini Serikali imefanya, tumeshazungumza na taasisi zote za fedha ambazo zinajishughulisha na utoaji wa mikopo, kufungua dirisha la mikopo kwa wajasiriamali wote na kuhakikisha kwamba kila anayefika pale anapata fursa sawa na mwingine ili kuboresha, kuwafanya Watanzania kubuni miradi na kuweza kupata mikopo ili waweze kujiongezea uchumi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kufatilia hilo, tunaendelea kufanya tathmini, pale ambako tutagundua bado kuna kundi ambalo halipati fursa tutaendelea kuweka utaratibu kupitia mifuko tuliyonayo hata pia ndani ya Serikali. Kwa hiyo, tutaendelea kuboresha utoaji mikopo kwa makundi yote, ili yeyote kutoka kwenye makundi hayo aweze kupata fursa ya kupata mitaji na kuendesha shughuli za kiuchumi, ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister