Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2020-2025 | Session 18 | Sitting 13 | Investment and Empowerment | Maswali kwa Waziri Mkuu | 4 | 2025-02-13 |
Name
Mwanaisha Ng'anzi Ulenge
Gender
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, awali ya yote niipongeze Serikali kwa kuanzisha East Africa Commercial and Logistics Centre pale Ubungo ili kuwawezesha Watanzania waliokuwa wakihangaika kwenda China na mitaji yao midogo kuweza kujipatia bidhaa zao hapa nchini.
Je, Serikali ina mkakati gani madhubuti wa kuwalinda, kukuza na kujenga ushindani wa wawekezaji wazawa ikiwemo kutoa preferences kwa wawekezaji wa ndani na kwa kuboresha mazingira ya uwekezaji wao na kuondoa vikwazo vinavyoweza kukwamisha uwekezaji na uzalishaji nchini ili zile bidhaa wanazoweza kuzalisha wao wazalishe badala ya kutegemea zile zinazoletwa na Wachina nchini?
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri Mkuu.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, sikuyapata vizuri maelezo ya awali ya swali lake yaliyojenga msingi wa swali zima, kwa hiyo, naomba arudie tena.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ulenge uliza swali vizuri, fupi lieleweke.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba je, Serikali ina mkakati gani madhubuti wa kulinda na kukuza uwekezaji wa wawekezaji wazawa ikiwemo kutoa preferences kwa wawekezaji wa ndani na kwa kuboresha mazingira ya uwekezaji wao ili zile bidhaa ambazo zinaweza kuzalisha nchini zizalishwe kuliko kutegemea kuletewa na Wachina?
Name
Kassim Majaliwa Majaliwa
Gender
Male
Party
CCM
Constituent
Ruangwa
Answer
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ulenge, Mbunge kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutoa hamasa kwa wawekezaji wa ndani ili waweze kuwekeza na waweze kuzalisha bidhaa badala ya kutegemea bidhaa kutoka nje kama ambavyo Mheshimiwa engineer ameeleza kutoka China.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja tumetengeneza mazingira nafuu ya uwekezaji wa Mtanzania kwa kupunguza kiwango cha kuwa mwekezaji, tumepunguza kutoka dola 100,000 kuja mpaka dola 50,000. Hii inamfanya sasa mwekezaji wa ndani kuweza pia kutafuta mtaji. Akishapata dola 50,000 anaingia kwenye orodha ya wawekezaji na akishaingia kwenye orodha ya wawekezaji mazingira yanamwezesha Mtanzania kuweza kuwekeza moja anapata mazingira rahisi ya kupata ardhi, mwenyeji anamiliki ardhi, lakini wageni wanapata hati tu ya kuwa wawekezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mbili; tumeona namna ambavyo bidhaa hizi zinavyoweza kuwekezwa na kufanyiwa biashara, hivyo tumetengeneza mazingira ya kumwezesha mfanyabiashara huyu au mwekezaji huyu kuendesha biashara yake katika mazingira rahisi. Tumeweka fursa na tumetengeneza mazingira ambayo yatamfanya afanye biashara vizuri, tumepunguza kodi, tumehakikisha kuwa hatua zile za kupata ardhi zinarahisishwa zaidi, lakini pia uendeshaji wa biashara anayoizalisha kama kuna biashara inazalishwa ndani ya nchi na kuna biashara aina hiyo hiyo inatoka nje ya nchi, ile inayotoka nje ya nchi tumeiongezea kodi ili kuipa nafasi hii kuingia kwenye masoko na kuweza kupata masoko yake vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira haya tumeendelea kuwahamasisha kwa Watanzania, lakini pia tumeweka masharti ya wawekezaji wa nje wanapokuja kuwekeza Tanzania lazima waambatane na Mtanzania kuwa mwekezaji mwenza ili Watanzania wapate nafasi ya kuwa wawekezaji wakubwa hapa ndani ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mazingira haya yote tumeendelea kufanya maboresho ya uwekezaji ndani ya nchi na kuhakikisha kuwa kila mwekezaji ambaye ni Mtanzania anafuata mazingira hayo ili kumwezesha kuwekeza kwa urahisi na kwa gharama nafuu na masoko yake tunayo ndani ya nchi, lakini na nchi jirani na tumeendelea kujenga mahusiano na nchi jirani kwa kuja kufanya biashara ili wawekezaji wetu waweze kuwekeza vizuri na kupata faida kwenye uwekezaji wao. (Makofi)
Copyright © Bunge Polis 2025. All Rights Reserved