Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 3 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2016-11-03

Name

Oran Manase Njeza

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Wakati tunaelekea kwenye msimu mwingine wa kilimo na mvua zimeshaanza kunyesha kwenye maeneo mengi ya nchi yetu likiwemo Jimbo langu la Mbeya Vijijini, lakini pembejeo za ruzuku za kilimo bado hazijawafikia walengwa. Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kuwa hizo pembejeo za ruzuku zinawafikia wakulima kwa muda muafaka?
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:- (Makofi/ kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wizara ya kilimo imeweka utarabu wa kusambaza pembejeo kwenye maeneo yetu kote nchini, pembejeo za mbegu na mbolea.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeamua msimu huu wa kilimo, kuanzia mwaka huu, kutumia taasisi inaitwa Tanzania Fertilizer Cooperation Company ili kupeleka mbolea, lakini pia mashirika mengine kusambaza pembejeo za aina nyingine. Mashirika haya tayari yameshakaa na Wizara ya Kilimo kwa pamoja ili kuweza kuratibu vizuri usambazaji wa pembejeo mpaka kwenye ngazi za vijiji na kuweza kuwafikia wakulima kabla ya msimu wa kilimo kuanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika mwezi uliopita tumeshatoa fedha kwa ajili ya kununua pembejeo na tumekabidhi taasisi zote ambazo nimezitaja ambazo pia zenyewe zinaweza kupata Mawakala kwenye ngazi ya Wilaya kule ili kuwafikishia wananchi kwenye ngazi ya vijiji na msimu huu wa kilimo utakapoanza, wakulima waweze kupata hizo pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote ambao kweli tumejikita kwenye kilimo kwamba, Serikali itaendelea kujitahidi kuhakikisha kwamba pembejeo zinawafikia wakulima kwa wakati na hasa wakati huu ambao mvua zimeshaanza kunyesha katika baadhi ya maeneo, kabla ya mazao husika kulimwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kusimamia na tutaendelea kutoa fedha zaidi ili tuweze kupeleka mbolea, mbegu za mazao ambayo yako kwenye orodha ya pembejeo kama ambavyo tumekusudia.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Oran Manase Njeza

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Question 1

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Napenda vilevile nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hatua ambazo Serikali imechukua kuhakikisha kuwa wakulima wetu wanapata pembejeo za ruzuku. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, napenda niulize swali dogo tu la nyongeza. Pamoja na hizo pembejeo za ruzuku, Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi tuliahadi kupunguza bei za pembejeo kwa msimu huu. Je, Serikali imechukua hatua gani au mkakati gani kuhakikisha kuwa kwa msimu huu pembejeo zote zinakuwa na nafuu kwa wakulima wetu? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli azma yetu Serikali ni kuhakikisha kwamba mkulima anapata pembejeo kwa gharama nafuu, lakini pia kwa wakati ili aweze kulima mazao mengi zaidi ili pia tuondokane na shida ya chakula nchini, lakini pia aweze kuuza mazao hayo pale ambako wanahitaji kuuza kwa ajili ya kuongeza uwezo wa kifedha ndani ya familia yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tumesema kwamba Serikali inatoa pembejeo kwa asilimia 25 ya mahitaji ya pembejeo na asilimia zilizobaki mkulima mwenyewe huwa anaweza kuendelea kuongeza ili kuweza kupata pembejeo; hii ni gharama nafuu, lakini tutaendelea kuangalia unafuu zaidi ili kumwezesha mkulima kupata pembejeo kwa gharama nafuu aweze kulima kilimo chenye tija kwa gharama nafuu vile vile.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nichukue jambo lako na tuendelee kuingia kwenye Serikali tuone utaratibu wa kuweza kupunguza gharama hizi ili wakulima wetu waweze kulipa fedha kidogo zaidi kuliko ilivyokuwa awali.