Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 3 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2017-02-02

Name

Suleiman Ahmed Saddiq

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mvomero

Primary Question

MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nina swali moja kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa waziri Mkuu, kwa kuwa mwaka 2016 miezi kama hii kulitokea upungufu mkubwa wa sukari nchini na Serikali ya Awamu ya Tano ilifanya jitihada kubwa sana kukabiliana na hali ile na hatimaye nchi yetu ikapata utulivu mkubwa katika suala zima la sukari.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba nikupongeze wewe na Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa mliyofanya mwaka 2016 katika suala zima la upungufu wa sukari nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kipindi hiki, viwanda vyetu vya ndani vinakamilisha msimu, vingine vinamaliza mwezi wa Tatu, vingine vinamaliza mwezi wa pili; na kwa kuwa vikikamilisha msimu, uzalishaji unaanza tena mwezi wa sita na kuendelea. Je, hali ilivyo sasa ya sukari nchini ikoje? Serikali imechukua juhudi gani kuhakikisha kwamba yale yaliyotokea mwaka 2016 hayatatokea?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saddiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka niwahakikishie Watanzania kwamba hakutakuja kutokea upungufu wa sukari, kwa sababu viwanda vyetu vya ndani vilishaanza uzalishaji na sasa vinaendelea na uzalishaji. Tunavyo viwanda vitano ambavyo tumevitembelea, tumehakiki utendaji kazi wake na uzalishaji upo na sukari ambayo inatumika nchini inatokana na uzalishaji huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaaamini kufikia mwishoni mwa msimu ambapo ni mwezi wa tatu mwaka huu wa 2017 tunaweza kuwa tumezalisha na kufikia malengo. Kwa sababu kwa taarifa za mwisho, mpaka mwishoni mwa Januari, uzalishaji kwa malengo waliokuwa wamejiwekea wamefikia asilimia 86. Asilimia iliyobaki inaweza kuzalishwa kwa kipindi kifupi kilichobaki.
Mheshimiwa Naibu Spika, na kama itajitokeza upungufu kwa sababu ya mahitaji ya sukari, pia kutozuia upandaji wa bei, Serikali itakuwa iko tayari kutafuta namna nzuri ya kupata sukari tukishirikiana na viwanda vyenyewe ikiwa ni mkakati wa kuvilinda viwanda vya ndani vinavyozalisha sukari ili viweze kuongeza uwezo wa uzalishaji wa sukari nchini. Huo ndiyo mpango wa Serikali.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Suleiman Ahmed Saddiq

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mvomero

Question 1

MHE. SULEIMAN A. SADDIQ: Mheshimiwa Waziri Mkuu, nakushukuru sana kwa majibu hayo. Kwa kuwa viwanda vya ndani vimejipanga, na kiwanda cha sukari Mtibwa ambacho kiko katika Jimbo la Mvomero na Wilaya ya Mvomero kimejipanga vizuri sana. Je, Serikali iko tayari kuvisaidia sasa viwanda hivi vya ndani ili viweze kukamilisha lengo la Taifa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saddiq kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba, wakati wote tumekuwa tukiendesha mazungumzo kati ya viwanda vyote vya ndani ikiwemo vya sukari, namna bora ya kuongeza uzalishaji wa bidhaa zao na bidhaa zenye ubora kwa namna ambayo Serikali inaweza na utayari wake iliyonao, kuvisaidia viwanda hivi kuweza kuzalisha zaidi. Kama ambavyo nimesema kwenye jibu la msingi, Serikali imekaa mara nyingi na wazalishaji wa sukari, kuona mwenendo wa uendeshaji wa viwanda vyao na uzalishaji wake, kupata changamoto zinazowakabili kwenye uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imedhamiria kulinda viwanda vya ndani na kusaidia uzalishaji mpana, tunao mpango na tumeandaa pia njia nzuri ya viwanda hivi kupata msaada wa kuendelea kuzalisha ikiwemo kupata mitaji, kupitia mabenki tuliyonayo na pia kuhamasisha wakulima wanaolima jirani ili waweze kuzalisha mazao yanayofanana na yale ili kuongeza uzalishaji. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kuwa pamoja na wazalishaji ili kuweza kuzalisha zaidi zao la sukari.