Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 10 Good Governance Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2017-04-20

Name

Freeman Aikaeli Mbowe

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Hai

Primary Question

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Mheshimiwa Waziri Mkuu nafikiri una hakiki kutokana na vyanzo vyako mbalimbali kwamba Taifa katika wakati huu linakumbwa na sintofahamu, hofu na taharuki nyingi zinazosababishwa mambo kadhaa.
Mheshimiwa Spika, moja na la msingi ambalo napenda kukuuliza ni kwamba kuna hofu kuhusu haki ya kikatiba ya kuishi na kupata hifadhi. Kuna hofu kuhusu haki ya kikatiba ya kupata na kutoa habari ambayo inaweza kuchagizwa kwa kiwango kikubwa na kukosekana kitu kama
uhuru wa Bunge kusikika kwa wananchi ambao wametutuma mahali hapa.
Mheshimiwa Spika, kuna hofu kuhusu watu kupotea, watu kutekwa na jambo hili limetawala sana kwenye mijadala katika mitandao na vyombo vya habari na mfano halisi ukiwemo kupotea kwa msaidizi wangu Ben Saanane ni miezi sita sasa Serikali haijawahi kutoa kauli yoyote, haielezi ni nini kinafanyika jambo ambalo linapelekea pengine kuamini aidha, Serikali haitaki kufanya uchunguzi ama imeshindwa kufanya uchunguzi. Mheshimiwa Waziri Mkuu unalipa Taifa kauli gani kuhusu hofu na taharuki hii ambayo imelikamata Taifa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbowe, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia kwamba Taifa lina hofu ya kikatiba kwenye maeneo kadhaa lakini pia amerejea michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge iliyokuwa inazungumzia suala la usalama wa nchi kwamba Taifa na Watanzania wana hofu na kwamba bado Serikali hatujatoa kauli.
Mheshimiwa Spika, kupitia majibu yangu lakini pia wakati wa bajeti yangu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, jambo hili mara lilipojitokeza tulitoa taarifa ya awali na mimi niliwasihi Watanzania kwamba Taifa letu kwanza ni Taifa ambalo kwa miaka mingi limekuwa na utamaduni mzuri wa watu kuheshimiana, watu kufuata misingi, kanuni, sheria na taratibu. Pia tunatambua kuwa kumetokea matukio mbalimbali kwa miaka mingi huko na matukio haya tumeendelea kuyaachia vyombo vya usalama kufanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa jambo ambalo limejadiliwa sana na Waheshimiwa Wabunge na hofu ambayo imekuwa ikielezwa kwamba Watanzania wana hofu, nilitumia nafasi yangu kuwasihi Watanzania kwanza waiamini Serikali yao kwamba moja kati ya majukumu ya Serikali yetu ni kuhakikisha Watanzania wanaishi kwa amani na kwa uhakika wa ulinzi wa wao wenyewe na mali zao wakati wote. Pia hata Serikali yetu nayo imeweka azma hiyo na kwamba jambo hili tunaendelea kuliimarisha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini kupitia michango hiyo pia hata Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi alieleza na mimi nikarejea kuimarisha hili kwamba Watanzania tunaomba mtupe muda, vyombo vyetu vinaendelea kufanya kazi ya kuchunguza ili tuweze kubaini ni nini hasa sasa kinatokea na ni kwa nini Watanzania wanafikia hapo kuwa na hofu. Haya yote huwezi kutoa matamko hadharani zaidi ya kuwasihi Watanzania kuwa watulivu na kutoa ushirikiano kwa Taifa na kwamba vyombo vyetu vinapofanya kazi kama tutaweza kueleza haraka maazimio yetu tunaweza tukapoteza njia nzuri ya kupata vyanzo vya kwa nini kasoro hizi zinajitokeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nirudie tena na nimsihi sana Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kwamba Serikali ipo na imesikia haya kutoka kwenye michango ya Waheshimiwa Wabunge. Naomba niwasihi tena Watanzania kuwa na imani na Serikali yenu kwamba tunaendelea na ufuatiliaji wa matukio yote yaliyozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge tuone kwa nini yanajitokeza, nani anasababisha kwa sababu vyanzo vya matatizo haya ni vingi na vinahitaji uchunguzi wa kina ili tuweze kujua hasa dosari iko wapi na tuweze kudhibiti. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wito wangu kwa Watanzania, tuendelee na utamaduni wa kutoa taarifa kwa vyombo vyetu pindi tunapojua kwamba hapa kuna jambo au linaandaliwa au limetokea na aliyesababisha ni fulani ili tuweze kuchukua hatua za papo kwa papo ili tuweze kunusuru watu wengine wasiweze kukubwa na matukio hayo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge mwenzangu na Kiongozi mwenzangu hapa Bungeni tuendelee kuipa muda Serikali kufanya ufuatiliaji wa jambo hili na baadaye tutakapogundua kabisa tutakuja kuwapa taarifa ili Watanzania wawe na uhakika na shughuli zao wanazoendelea nazo. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Freeman Aikaeli Mbowe

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Hai

Question 1

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kukiri kwamba Taifa letu lina historia ya watu kuheshimiana, ni jambo jema na ni kweli tumekuwa na historia hiyo na hofu ninayoizungumza ndiyo hiyo hiyo kwamba ustaarabu na utamaduni huo unaonekana kupotea kwa kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na Serikali kututaka tuiamini, tuipe muda lakini hapa tunazungumzia kifo au kupotea kwa mtu. Jambo hili linazua hofu kwa familia na kwa Watanzania wote katika ujumla wake. Nina hakika mtu yeyote mwenye mapenzi mema na nchi yetu anaona jambo hili linataharuki kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni utamaduni wa nchi yetu kushirikiana na mataifa mbalimbali katika maeneo


mbalimbali na kwa sababu mataifa yanatofautiana katika uwezo wa kufanya tafiti, uwezo wa kufanya uchunguzi na kipekee nikizungumza Uingereza ambayo tuna mahusiano mazuri nao wametumika maeneo mbalimbali duniani pale ambapo panaonekana pana uzito wa kiuchunguzi, taasisi yao ya Scotland Yard ina uwezo wa kusadia. Kama ambapo ilifanyika Kenya wakati amepotea na ameuwawa katika mazingira ya kutatanisha Robert Ouko aliyekuwa Kiongozi katika Jamhuri ya Kenya watu wakaomba Serikali kama imeshindwa kuchunguza iombe Scotland Yard watoe msaada na wana utaalam mkubwa katika forensic investigation na waliweza kufanya hivyo na wakatoa taarifa yao iliyokuwa sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na mazingira hayo basi kwa nini Serikali isitoe kauli kwa sababu miezi sita ni mingi na hofu inazidi kuwa kubwa, kwa nini Serikali isione umuhimu wa ku-engage Scotland Yard iweze kuja kusaidiana na jeshi letu na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ili kuonyesha ile nia njema kujaribu kuchunguza jambo hili kwa haraka kwa sababu wenzetu tukiri wana teknolojia ya ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile Waziri Mkuu atakumbuka katika uhuru na haki niliyoizungumzia hapa hajatoa kauli yoyote kuhusu kurushwa kwa Bunge live. Hebu tupe kauli ya Serikali basi turejee utamaduni wetu wa Kitanzania Bunge hili lisikike kwa wananchi ambao wametutuma hapa ndani. Tunaomba kauli ya Serikali kwenye hilo vilevile.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Mbowe, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, najua kuna maswali mawili, la kwanza ni lile la kwa nini Serikali isishirikiane na mataifa mengine katika kufanya uchunguzi wa matukio kadhaa ndani ya nchi. Kwanza, nataka nikuthibitishie kwamba Taifa letu linayo mahusiano na mataifa kadhaa ambayo tunashirikiana kwenye mambo mbalimbali ikiwemo na mambo ya kiulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na matukio haya yanayojitokeza huku ndani, nikuhakikishie pia Taifa letu lina uwezo wa ndani wa kufanya ufuatiliaji wa kutambua matukio haya ya awali ya mtu kufariki au kutoweka mahali. Baada ya familia husika kutoa taarifa tunaweza tukafanya uchunguzi huo na baadaye tukaweza kubaini vyanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nimesema yote haya lazima mtuamini Serikali kwamba tunayo nia njema kabisa ya kutambua vyanzo na namna ya kudhibiti uendelezaji wa matukio yote ambayo yamejitokeza nchini.
Mheshimiwa Spika, ni kwamba Serikali haina kikomo cha uchunguzi kutegemea na nature ya tatizo lenyewe. Familia ya mtajwa aliyetangulia mbele za haki au vinginevyo hata sina uhakika, tunaweza kusema kwamba uchunguzi huu utakapokamilika taarifa itatolewa. Ingawa umesema kwamba ni miezi sita lakini kama ambavyo nimesema kwenye jibu la msingi kwamba itategemea kama vyombo vyetu vinapata msaada kutoka kwenye jamii na vyanzo vingine


na teknolojia ambayo tunaitumia kuweza kufikia hatua ya kupata majibu ya uchunguzi ambao tunautoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado naendelea kutoa kauli ya kuwaomba Watanzania kuwa watulivu na kuamini jeshi letu kwamba linafanya kazi. Vilevile sisi Serikali jambo hili ni letu, Watanzania watupe ushirikiano wa kutuhabarisha vyanzo vya matukio haya ili tuweze kufikia hatua muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge alitaka pia kupata ufafanuzi wa jambo la pili ambalo lilishazungumzwa na Bunge lililopita na maamuzi yalishatolewa ya kwamba Bunge letu litakuwa limeweka utaratibu wa namna ya kuwafikishia matangazo Watanzania. Utaratibu huo unaendelea na Watanzania wanapata matangazo kupitia utaratibu ambao tumeuandaa. Kwa hiyo, tutaendelea kuboresha kadiri ambavyo tunaona inafaa ili kuweza kuwafikishia ujumbe Watanzania. Ahsante sana.