Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 22 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2017-05-11

Name

Kunti Yusuph Majala

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunapoingia kwenye chaguzi vyama pamoja na wagombea huwa wanawaahidi wananchi ili waweze kuwaamini na kuweza kuwapa nafasi katika nafasi mbalimbali wanazogombea. Mnamo tarehe 5 Oktoba, 2015 mgombea Urais kupitia Chama cha Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia katika uwanja wa Barafu Manispaa ya Dodoma alikutana na mabango mbalimbali ya wananchi wa Manispaa ya Dodoma wakilalamikia suala la CDA na mgombea Urais Mheshimiwa John Pombe Magufuli aliwaahidi wakazi wa Manispaa ya Dodoma endapo watampatia kura za kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jukumu lake la kwanza ni kuifuta CDA.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, wakazi wa Manispaa ya Dodoma wanapenda kujua ni lini ahadi hii ya Mheshimiwa Rais itakwenda kutekelezwa? Ahsante

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika naomba kujibu swali la Mhesimiwa Kunti, Mbunge wa Dodoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa anafanya ziara maeneo mbalimbali amekuwa akitoa ahadi kadhaa. Nataka nirudie kusema tena kwa Watanzania kwamba ahadi ambazo Mheshimiwa Rais ameziahidi tutajitahidi kuzitekeleza kwa kiasi kikubwa ikiwemo na uboreshaji wa Mji wa Dodoma, pia moja ya ahadi yake ilikuwa ni kwamba katika awamu yake hii kufikia mwaka 2020 atahakikisha Serikali inahamishia Makao yake Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ikiwa ni moja kati ya mambo ambayo aliyaahidi na tumeyatekeleza, mbili kwa kuwa tayari Serikali imehamia Dodoma lazima sasa tuandae utaratibu wa uboreshaji wa mazingira ya Mji wa Dodoma ili utawala wake, uendeshaji uweze kuwa rahisi ikiwemo na kupitia sheria mbalimbali zilizoiunda CDA, kuzifanyia mapitio na kuziboresha ili tuweze kuachana na CDA tuwe na mfumo ambao utatoa nafasi kubwa ya kukaribisha watu wa kawaida, wawekezaji na kuitumia ardhi iliyopo kwenye Manispaa katika kuwekeza au vinginevyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa nikiri kwamba kwa Sheria ya CDA huwezi kuleta mwekezaji hapa kwa sababu ni CDA pekee ndiyo imepewa ardhi hii na wao ndiyo waliopewa hati na ardhi Makao Makuu. Kwa hiyo wao wasingeweza kutoa hati kwa wananchi wanaojenga au wanaowekeza hapa, ili kuwapa nafasi wananchi kuwa na hati ya umiliki wa ardhi lazima tufute Mamlaka ya CDA ili tuweze kutumia Sheria ya Ardhi katika kutoa ardhi iliyopo hapa ili tuweze kukaribisha wawekezaji na uboreshaji wa mpango ambao sasa tumeukamilisha kuhamia Makao Makuu Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nikutoe wasiwasi kwamba sasa tunafanya mapitio na Mheshmiwa Rais ameshatoa maagizo Tume imeshaundwa inafanya mapitio ya namna bora ya kuifuta CDA lakini kupitia sheria zilizoiweka CDA, hiyo ndiyo hatua ambayo tumeifikia na katika kipindi kifupi tutakuwa tumeshatoa taarifa. Ahsante.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Kunti Yusuph Majala

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Question 1

MHE. KUNTI Y. MAJALA: heshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mkiwa bado kwenye huo mchakato wa kwenda kupitia sheria na mambo kadha wa kadha, hata wewe pia unafahamu kuwa changamoto kubwa iliyopo baina ya wakazi wa Manispaa ya Dodoma na CDA, nini tamko lako kwa CDA kuhusiana na bomoabomoa zinazoendelea bila wananchi hao kulipwa stahiki zao?

Jambo la pili, endapo hamtakamilisha huo mchakato, mnawaambia nini Watanzania wa Manispaa ya Dodoma kwamba ahadi iliyotolewa ilikuwa ya uongo na kuwarubuni Watanzania ili mpate kura then muwapotezee? Kama msipofanya hivyo mnawaambia Watanzania wasiwachague tena kwa sababu mmekuwa na ahadi za uongo zisizotekelezeka? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimwambie usiwe na mashaka ya utekelezaji wa Ilani zetu na kwamba umeanza kutanguliza majibu ya wananchi msiwachague tena hilo siyo lako, wewe subiri tutekeleze ahadi zetu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote wa Mkoa wa Dodoma wakiwemo na wananchi wa Manispaa, jambo muhimu hapa ni kufanya maboresho ya Mji wa Dodoma ambako ni Makao Makuu ya Serikali. Kama ambavyo nimeeleza kwenye maelezo yangu ya msingi kwamba tayari Tume imeshaundwa wanaendelea kuharakisha zoezi hilo la kuhakikisha kwamba tunaondoka kwenye sheria iliyounda CDA ili kurudi kwenye sheria tuweze kuifanya CDA iweze kufanya kazi zile ambazo zitampa mwananchi haki ya kuweza kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo swali ambalo limesema wale ambao wanabomolewa na CDA, sasa hili ni lazima tufanye mapitio CDA utaratibu wanaoutumia, wanabomoa kwa ajili ya nini na je, maeneo hayo na wale wanaobomolewa wanatakiwa kupata stahili ya namna gani. Kwa sababu sheria tuliyonayo inamtaka popote ambako unataka kupatumia kwa kuondoa mali ambayo mwananchi amewekeza lazima uilipie fidia.

Kwa hiyo sheria ipo, lazima tuone tufanye mapitio tuone CDA sasa wanaendesha operation wapi na wanalipa au hawalipi ili tuweze kujua kama hawalipi kuna sababu gani za msingi za kutolipa, lakini haki ya kulipwa ipo pale na ninaamini CDA ipo ofisini kwangu, kwa hiyo nitafanyia mapitio halafu nitakupa taarifa.