Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 43 Good Governance Ofisi ya Rais TAMISEMI. 365 2016-06-15

Name

Rose Kamili Sukum

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. EZEKIEL M. MAIGE (K.n.y MHE. ROSE K. SUKUM) aliuliza:-
Serikali ina utaratibu wa kutoa fedha kwa ajili ya shule za bweni nchini. Kwa kipindi cha kuanzia tarehe 31/08/2013 hadi tarehe10/02/2014 Halmashauri ya Hanang ilipokea kutoka Serikali Kuu kiasi cha shilingi 508,779,500 kwa ajili ya chakula cha shule za bweni. Taarifa zinaonesha kwa fedha zilizotumika kununua chakula ni shilingi 225,585,000 kwa takwimu hizo bakaa ni shilingi 283,194,500 kwa mujibu wa Mkaguzi, bakaa hiyo haionekani kwenye account yoyote benki.
(a) Je, fedha hizo zinarudishwa Hazina bila ya kuwa na uwepo wa nyaraka zozote toka Halmashauri kuonesha muamala unavyofanya kazi?
(b) Je, kama fedha hizo hazikurudishwa Hazina nani anaweza kuidhinisha matumizi bila ya mpango wake kupitishwa na Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri?
(c) Je, kama fedha zimetumika bila kupangiwa na Kamati halali, ni kwa nini wahusika bado wanaendelea kuwa ofisini bila ya kufunguliwa mashtaka ya wizi wa kuaminika?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Kamil Sukum, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014 Halmashauri ya Wilaya ya Hanang iliidhinishiwa shilingi 225,585,000 kwenye ruzuku ya uendeshaji wa shule za msingi kwa ajili ya chakula cha wanafunzi kwa shule za bweni za Katesh, Balangdalalu, Bassodesh na Gendabi. Fedha zilizotolewa zilikuwa ni shilingi 508,779,500 zikiwa ni ziada ya shilingi 283,194,500. Fedha hizo hazikurejeshwa Hazina badala yake zilibadilishwa matumizi na kutumika kwa ajili ya vifaa vya shule na ukarabati wa shule hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizo zilizoombewa kibali cha kubadili matumizi ili zitumike kununua vifaa vya shule na ukarabati wa mabweni. Hata hivyo ni kweli maombi hayo hayakujadiliwa katika Kamati ya Fedha na Mipango na kwa mantiki hiyo utekelezaji wa jambo hilo ulikiuka misingi na utaratibu wa uendeshaji wa Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na makosa hayo Mkurugenzi wa Halmashauri amesimamishwa kazi pamoja na Watumishi wengine wanne wakiwepo Afisa Mipango Wilaya, Mweka Hazina Wilaya na Wahasibu wawili ili kupisha uchunguzi. Aidha, Baraza la Madiwani limeelekeza fedha hizo zirejeshwe kupitia mapato ya ndani na tayari shilingi milioni 130 zimepelekwa kwenye akaunti ya vijiji vya Gendabi, Bassodesh, Katesh na Balangdalalu.