Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 43 Energy and Minerals Wizara ya Madini 372 2016-06-15

Name

Sebastian Simon Kapufi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Mjini

Primary Question

MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza:-
Dhahabu ni kati ya madini yanayozalishwa na wachimbaji wadogo wadogo Mkoani Katavi; na kumekuwepo na suala la asilimia hafifu ya dhahabu ya Mpanda Kati ya 60% hadi 90%. Uhafifu huu ulitokana na ukweli kwamba sehemu ya asilimia ni madini mengine kama fedha, shaba na kadhalika, lakini katika mauzo wachimbaji wamekuwa wakilipwa thamani ya dhahabu tu.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwawezesha wachimbaji hawa kwa kuwapatia teknolojia sahihi ya kutofautisha dhahabu, shaba na fedha ili kuongeza thamani na pato halisi kwa wachimbaji hao na kuinua Pato la Taifa?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa, mbali na dhahabu (gold ore) katika maeneo ya Mpanda huwa na madini mengine kama vile fedha, shaba pamoja na madini ya risasi. Kwa upande wa wachimbaji wadogo wa dhahabu nchini, kiwango cha uchenjuaji wa dhahabu huwezesha kuzalisha dhahabu kwa wastani wa asilimia 60 tu. Sababu kubwa ni pamoja na mitambo duni ya uchenjuaji inayotumika; kuanza uzalishaji kabla ya kufanya utafiti wa kujua aina ya mitambo inayotumika, lakini pia kiwango duni cha usagaji mbale.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona umuhimu sasa wa kuwawezesha wachimbaji wadogo kwa kuwapatia teknolojia sahihi ya kutofautisha dhahabu, shaba na fedha kwa ajili ya mafunzo. Kuanzia mwezi Septemba, 2016, Serikali kupitia Wizara yangu itaanza kujenga vituo vya mfano pamoja na kutoa mafunzo ya uchenjuaji madini hususan dhahabu katika Mikoa ya Geita, Katavi pamoja na Mara.
Kadhalika madini ya chokaa katika Mkoa wa Tanga, madini ya bati katika Mkoa wa Kagera na madini ya chumvi katika Mkoa wa Lindi ikiwa ni pamoja na madini ya vito katika Mkoa wa Ruvuma. Vituo hivi vitasaidia sana kuongeza viwango vya uchenjuaji madini hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sasa pia niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuwashauri wachimbaji wadogo katika maeneo yao kutumia taasisi zetu za Serikali ikiwa ni pamoja na STAMICO ambalo hushughulikia masuala ya wachimbaji wadogo, Chuo cha Madini Dodoma, Vyuo Vikuu vya Dodoma na Dar es Salaam na Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ili kuwafanyia utafiti na kuwashauri mambo yanayofaa kwa ajili ya uchimbaji na uchenjuaji wa tija.