Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 13 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 68 2023-11-03

Name

Emmanuel Lekishon Shangai

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Primary Question

MHE. EMANNUEL L. SHANGAI aliuliza:-

Je ni sheria ipi inawaruhusu Watumishi wa TANAPA, TAWA na NCAA kutoza mifugo shilingi 100,000 pindi iingiapo hifadhini?

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emannuel Lekshon Shangai, Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taasisi za Uhifadhi za TANAPA, NCAA na TAWA zinaongozwa na Sheria mahususi za kusimamia rasilimali za wanyamapori. Mathalan, Sheria ya TANAPA Sura 282 Kifungu cha 28(1)(a) kama kilivyorekebishwa na Sheria ya Marekebisho Mbalimbali (Na. 11) ya mwaka 2003 ambayo imeongeza kifungu 20A cha Sheria hiyo kwa kuwapa mamlaka watumishi wa TANAPA kutoza faini isiyozidi shilingi 100,000 kwa kila kosa pale mkosaji anapokiri na kukubali kwa maandishi kulipa faini kwa kosa husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kifungu cha 116 cha Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori, Sura ya 283 hutumika katika kutoza faini pindi mifugo inapoingizwa kinyume cha sheria, ndani ya mapori ya akiba. Kifungu hiki kimebainisha utaratibu wa kulipa faini ambapo mkosaji atalipa faini mara baada ya kukubali na kukiri kosa. Aidha, sheria imeelekeza kuwa kiwango cha faini hakitapungua shilingi 200,000 na hakitazidi shilingi 10,000,000. Mkosaji hukiri kosa kwa maandishi na kulipa faini hiyo, na endapo hatakuwa tayari kulipa faini, hufikishwa Mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Wananchi kwa ujumla kuwa Serikali itaendelea kuhifadhi na kusimamia rasilimali za wanyamapori kwa kushirikiana na jamii. Hivyo, tunawaomba wote watoe ushirikiano katika kufanikisha jukumu hilo na kuwasihi wazingatie sheria ili kuepusha migongano isiyo ya lazima baina yao na Wahifadhi.