Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 6 Community Development, Gender and Children Ofisi ya Rais TAMISEMI. 63 2016-02-02

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:-
Malengo ya TASAF III ni kunusuru kaya maskini hapa nchini na kutengeneza miundombinu kutokana na mahitaji na uibuaji wa kaya maskini unaofanywa na wananchi kwenye mikutano ya hadhara:-
(a) Je, ni vigezo gani vinatumika kuondoa kaya zilizopendekezwa kwenye mradi na kubakiza kaya chache wakati malengo ya kaya zinazohitajika, wananchi wameshapewa tangu awali?
(b) Katika Wilaya ya Kaliua, vijiji vilivyoingia kwenye miradi ni 54 tu, wakati katika vijiji vyote kuna kaya maskini sana. Je, ni lini Serikali itapeleka Mpango wa TASAF III kwenye vijiji vilivyobakia kwenye Wilaya hiyo?

Name

George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kujibu swali lililoulizwa na Mheshimiwa Magdalena Hamisi Sakaya, Mbunge wa Jimbo la Kaliua, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, utambuzi wa Kaya za walengwa unapitia mchakato wenye hatua zifuatazo:-
Hatua ya kwanza ni Mpango wa kunusuru kaya maskini kutambulishwa kijijini na wataalam wanaotoka katika Halmashauri husika kwa kusimamiwa na Uongozi wa kijiji na kisha kuweka vigezo vya kaya maskini.
Pili, wakusanya taarifa wanachaguliwa kutoka miongoni mwa vijana wanaoishi kijijini hapo na kupitia nyumba kwa nyumba ili kuorodhesha kaya ambazo zinakidhi vigezo vilivyoainishwa na Mkutano Mkuu wa Kijiji.
Tatu, orodha ya kaya zilizoorodheshwa na timu ya wakusanya taarifa kusomwa mbele ya Mkutano wa Kijiji na baada ya hapo jamii hujadili majina yaliyoorodheshwa na kufikia muafaka. Kaya ambazo jamii inaona hazistahili, huondolewa kwenye orodha na Kaya ambazo hazikuwa zimeorodheshwa, huingizwa kwenye orodha.
Nne, kutokana na orodha hiyo ambayo imeandaliwa, kaya hizo hujaziwa dodoso maalum linaloandaliwa na TASAF Makao Makuu kwa lengo la kupata taarifa zaidi za kaya.
Tano, dodoso hilo lililojazwa huchambuliwa kupitia mfumo maalum wa kompyuta ili kupata kaya maskini sana ambazo zinakidhi vigezo kulingana na taratibu za mpango huo.
Mwisho, baadhi ya kaya ambazo hazifikii kiwango cha alama zinazotakiwa huondolewa katika orodha.
Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya kaya maskini zilizotambuliwa na kupitishwa kwenye Mkutano wa Kijiji mara nyingine zimejikuta zimetolewa wakati wa kuchambua taarifa kutokana na taarifa ambazo mwanakaya aliyedodoswa anakuwa amezitoa wakati wa kujaziwa dodoso.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Kaliua, vijiji 54 vilivyoingizwa kwenye mpango huu wa TASAF ni asilimia 70 ya vijiji vyote ndani ya Wilaya hiyo. Hii ni kwa mujibu wa taratibu za mpango ambapo kila Halmashauri iliyomo ndani ya mpango, siyo Kaliua pekee, imeingiza wastani wa asilimia 70 tu ya vijiji au mitaa iliyomo ndani ya Halmashauri. Asilimia 30 ya vijiji na mitaa iliyosalia katika Halmashauri zote imepangwa kufikiwa katika mwaka 2016.
Serikali ilitoa maagizo hayo ili kuweza kufikia Vijiji, Mitaa, Shehia zote zilizobakia; na kwa upande wa Vijiji, Mitaa na Shehia zilizoanza ndizo zilizokuwa na hali mbaya zaidi. Kabla ya kuanza utekelezaji, takwimu za umasikini zilichukuliwa katika Vijiji, Mitaa na Shehia zote na kuorodheshwa kuanzia ambazo ni masikini sana mpaka zenye unafuu.