Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 4 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 55 2016-09-09

Name

Prof. Norman Adamson Sigalla King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Primary Question

MHE. DEO K. SANGA (K.n.y. MHE. PROF. NORMAN A. S. KING) aliuliza:-
Shamba la Mifugo la Kitulo lililoko Wilaya ya Makete lilianzishwa kwa madhumuni ya kuwezesha wananchi kupata ndama na maziwa kwa ajili ya kukuza uchumi wao, lakini cha kusikitisha, uzalishaji wa ng‟ombe katika shamba hilo kwa sasa umepungua sana kutokana na Serikali kushindwa kusaidia kuimarisha shamba hilo:-
Je, Serikali inafanya jitihada gani kuimarisha shamba hilo ili liweze kusaidia wananchi wa Makete na Mikoa ya jirani kupata ng‟ombe na kukuza uchumi wao?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Norman Sigalla King, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, shamba la kuzalisha mifugo la Kitulo ni kati ya mashamba matano ya kuzalisha mifugo yanayomilikiwa na kuendeshwa na Wizara kwa lengo la kuzalisha mifugo bora kwa ajili ya kuwauzia wafugaji kwa bei nafuu. Shamba hili huzalisha ng‟ombe wa maziwa aina ya Friesian pamoja na maziwa, katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2011/2012 hadi 2015/2016, jumla ya mitamba 365 na madume bora 515 yalizalishwa na kuuzwa kwa wafugaji katika Mikoa ya Mbeya, Njombe, Iringa na Ruvuma. Kati ya mitamba hiyo, 40 iliuzwa kwa wafugaji wa Wilaya ya Makete.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika kipindi hicho jumla ya lita 1,963,241 zilizalishwa katika shamba hili na kuuzwa. Shamba hili pia linaendelea kutumika kutoa mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi na wafugaji kutoka vijiji jirani vikiwemo vya Wilaya ya Makete. Katika kipindi hicho, wanafunzi 930 kutoka vyuo mbalimbali vya mifugo hapa nchini na wastani wa wafugaji 250 walipata mafunzo ya vitendo kupitia shamba hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuliimarisha na kuliendeleza shamba hili kwa kuboresha miundombinu ya shamba ikiwepo maeneo ya malisho kwa kupanda na kuwekea mbolea hekta 500 za malisho, kukarabati kilometa 15 za mfumo wa maji, kukarabati na kuweka umeme nyumba 13 za watumishi, kuongeza ubora wa ng‟ombe waliozalishwa na kununua madume bora ya Friesian 12 na kutumia teknolojia ya uhimilishaji wa mbegu zilizotengenezwa kijinsi, kununua mitambo na mashine ikiwa ni pamoja na mashine moja ya kukamulia na tenki moja la kubeba maziwa, magari mawili pamoja na trekta mbili na vifaa vyake kwa ajili ya kuboresha na kurahisisha kazi za shamba.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hizi zimetekelezwa kwa kutumia fedha zinazozalishwa shambani kila mwaka na zinazotolewa kupitia bajeti ya Wizara. Katika mwaka wa fedha, 2016/2017 jumla ya shilingi milioni 105 zitakazozalishwa shambani na zilizotengwa kupitia bajeti ya Wizara zimepangwa kutumika katika kuimarisha na kuendeleza shamba hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inawahamasisha wananchi wa Makete kutumia huduma ya uhimilishaji ili waweze kuzalisha ndama bora kutokana na mifugo yao wenyewe.