Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 6 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 65 2016-02-02

Name

Risala Said Kabongo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RISALA S. KABONGO aliuliza:-
Hifadhi za Mikoa ya Kusini za Mikoa ya Kusini za Ruaha, Kitulo, Udzungwa, Mikumi na Katavi na maeneo mengine ya kihistoria husifika sana kwa vivutio vyake, lakini kutembelewa na idadi ndogo sana ya watalii na hivyo kuwa na mapato madogo na kuwa tegemezi kwa Hifadhi za Mikoa ya Kaskazini:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa muda mfupi na mrefu wa kuongeza idadi ya wageni katika hifadhi hizo?
(b) Je, Serikali ina mikakati gani ya kuboresha miundombinu ya barabara, malazi na viwanja vya ndege katika hifadhi hizo kwa matumizi ya watalii?
(c) Je, kwa nini Serikali isishirikiane na wawekezaji binafsi ili kuwekeza katika maeneo ya utalii kwenye Hifadhi hizo za Mikoa ya kusini?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Risala Saidi Kabongo, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa na Shirika la USAID, ilifanya upembuzi yakinifu na kuandaa mikakati ya kuendeleza na kutangaza utalii kwenye eneo la Kusini mwa Tanzania mwaka 2015. Ili kutekeleza mikakati hiyo, Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia itatekeleza mradi utakaojulikana kama Tanzanian Resilient Natural Resources Management for Growth. Mradi huu ambao utatekelezwa kwa miaka sita, umepangwa kuanza kutekelezwa Januari, 2017 na utagharimu takribani Dola za Kimarekani milioni 100.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zitakazotekelezwa na mradi huo ni pamoja na kuimarisha uhifadhi wa mazingira, kuendeleza utalii na kuwezesha wananchi kunufaika na utalii. Mradi huu utahusisha pamoja na mambo mengine, uimarishaji wa miundombinu ya utalii hasa barabara, viwanja vya ndege na huduma za malazi. Vilevile kutengeneza circuit ya utalii kwa upande wa Kusini ili mgeni aweze kutembea au kutembelea eneo au hifadhi zaidi ya moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada mbalimbali zimefanywa na zinaendelea kufanywa ili kuboresha shughuli za utalii Kusini na Magharibi mwa Tanzania. Jitihada hizo ni pamoja na kuimarisha barabara toka Tunduma kwenda Mpanda kupitia Sumbawanga kwa kiwango cha lami ambayo itaziwezesha hifadhi za Katavi na Mahale kufikika kwa urahisi.
Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika, ujenzi wa barabara ya Sumbawanga hadi Kasanga kwa kiwango cha lami ambayo itapanua wigo wa wataalii kutembelea Ziwa Tanganyika pamoja na vivutio vingine nje ya hifadhi kama vile maporomoko ya Kalambo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada nyingine ni kuimarisha na kuboresha viwanja vya ndege vya Songwe, Kigoma na Mpanda ambavyo vitasaidia kufikika kwa maeneo ya vivutio yaliyotajwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ukarabati wa barabara itokayo Kigoma kuelekea Kusini hadi Kaliya, Namwese ambayo itaunganisha Mkoa wa Katavi, hivyo kuwezesha watalii kufika Mahale kwa urahisi zaidi. Shirika la Hifadhi za Taifa litaunganisha Hifadhi ya Mikumi na Pori la Akiba la Selous kwa barabara itakayopitika mwaka mzima ili kuwezesha watalii wengi wanaofika Selous kufika Mikumi, kutembelea maeneo hayo kwa urahisi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, vivutio vya Utalii Kusini mwa nchi vitaendelea kutangazwa na taasisi zilizo chini ya Wizara na kuimarisha Ofisi ya Kanda ya Iringa Mjini.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuvutia wawekezaji binafsi kutoa huduma mbalimbali za watalii ikiwemo malazi, ambapo vibali 11 vimetolewa kuwekeza kwenye huduma za malazi katika Hifadhi za Ruaha, Mikumi, Katavi na Mahale. Uwekezaji huo ambao upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji utaongeza jumla ya vitanda 544.