Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 15 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 38 2024-04-05

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-

Je, kwa nini ujenzi wa Barabara ya Bukiko hadi Bwisya kupitia Katende inayosimamiwa na TARURA haukamiliki kwa zaidi ya miaka miwili sasa?

Name

Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. ZAINAB A. KATIMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa sababu leo ndio siku ya kwanza nasimama mbele ya Bunge lako Tukufu kwa mara ya kwanza kama Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba nichukue dakika moja kutoa maneno ya utangulizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na siha njema mpaka wakati huu. Kipekeee naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani yake kubwa kwangu kwa kuniteua katika nafasi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Namuahidi Mheshimiwa Rais nitafanya kazi kwa bidii, weledi na uadilifu mkubwa ili kumsaidia majukumu yake na kutimiza maono yake kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii pia kukushukuru wewe kama mlezi wetu sisi Wabunge, kwa nasaha zako, kwa mafunzo yako ambayo yamenijenga mimi kiuongozi, lakini pia katika maisha yangu binafsi, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa ushirikiano mkubwa ambao wamenionesha. Kwa heshima kubwa na unyenyekevu niwaombe ushirikiano zaidi sasa ili kwa pamoja tuweze kushirikiana kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutimiza maono yake kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii adhimu pia kuwashukuru akinamama wote na wapigakura wangu wa Mkoa wa Kigoma kwa kuendelea kunipa ushirikiano mkubwa unaonipa utulivu katika kazi zangu. Baada ya kusema maneno hayo ya utangulizi, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini ilifanya matengenezo ya kufungua upya Barabara ya Bukiko hadi Bwisya kupitia Katende kilometa 7.54 kwa gharama ya shilingi milioni 141.2. Fedha hizo zilitekeleza kazi za ufunguzi wa barabara na kuunda tuta la barabara kilometa 7.54, ujenzi wa madaraja madogo matatu na ujenzi wa mistari minne ya madaraja madogo. Kazi zote zilikamilika kwa mujibu wa mkataba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, Serikali imeweka katika mipango yake ya Mwaka wa Fedha 2024/2025, kufanya matengenezo ya kawaida na kujenga madaraja madogo mawili kwa gharama ya shilingi milioni 30.16 ili barabara iweze kupitika wakati wote. (Makofi)