Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 37 Education, Science,Technology and Vocational Training, Ofisi ya Rais TAMISEMI. 304 2016-06-06

Name

Tunza Issa Malapo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA (K.n.y MHE. TUNZA I. MALAPO) aliuliza:-
Dhana ya elimu ni majumuisho ya mambo mengi sana ikiwemo matibabu ya huduma ya kwanza, gharama za umeme, maji, vyakula (kwa shule za bweni), posho za walimu (part time) pamoja na zana za kufundishia zisizohifadhika kwa muda mrefu; na nyingi kati ya gharama hizo zilikuwa zinatatuliwa mashuleni na Wakuu wa Shule kwa kutumia ada na michango waliyokuwa wanatoza wanafunzi.
Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha ufanikishwaji wa dhana hii ya elimu bure bila kuanzisha migogoro mipya kati ya wakuu wa shule, walimu, wazazi pamoja na wanafunzi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya utoaji wa elimu bila malipo inatokana na Sera ya Elimu na mafunzo ya mwaka 2014 inayoelekeza utaratibu wa ugharamiaji wa elimu ya awali kuwa ya lazima kuanzia shule za msingi hadi sekondari kidato cha nne.
Mheshimiwa Naibu Spika, elimu msingi bila malipo inazingatia uendeshaji wa shule bila ada wala michango ya aina yoyote ya lazima kutoka kwa wazazi au walezi wa wanafunzi. Hata hivyo, elimu bila malipo haiondoi dhamira ya uzalendo kwa jamii ya kushiriki kwa hiari kuchangia kwa hali na mali katika kuleta maendeleo ya elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kupeleka shilingi bilioni 18.777 kila mwezi kwa ajili ya kugharamia mpango huu. Fedha hizo zinatumika kugharamia mitihani ya Taifa, chakula cha wanafunzi wa bweni, ada ya mwanafunzi kwa shule za kutwa na bweni na fedha za uendeshaji wa shule za msingi na sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga ili kuhakikisha kuwa utoaji wa elimu bila malipo ambao umeshaanza kwa shule zote za umma nchini hausababishi migogoro kati ya wakuu wa shule, walimu, wazazi pamoja na wanafunzi. Ili kuhakikisha hilo halitokei Serikali imetoa miongozo mbalimbali katika mikoa yote inayofafanua kuhusu utekelezaji wa mpango huo.