Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 36 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 299 2016-06-03

Name

Dr. Immaculate Sware Semesi

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SIKUDHANI Y. CHIKAMBO (K.n.y. MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI) aliuliza:-
Sekta ya maliasili na utalii ni rasilimali inayobeba uchumi wa Tanzania, ikitumika vizuri kwa uendelevu, italeta maendeleo katika jamii na uchumi wa nchi kwa ujumla:-
(a) Je, ni lini Serikali itaanza kuipa kipaumbele sekta ya utalii?
(b) Je, ni lini Serikali itaboresha mazingira ya kazi ya askari wanyamapori?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Immaculate Sware Semesi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba sekta ya maliasili na utalii inatoa mchango mkubwa na kubeba uchumi wa Tanzania. Kwa mfano, sekta hii imechangia takribani asilimia 25 ya fedha zote za kigeni nchini katika kipindi cha miaka mitatu mfululizo yaani 2012/2013 – 2014/2015 na hivyo kuchangia zaidi ya asilimia 17 ya Pato la Taifa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Utalii imechangia pia katika ajira nchini ambapo takribani ajira 500,000 za moja kwa moja ambayo ni takribani asilimia 11 ya ajira zote na ajira takribani 1,000,000 zisizo za moja kwa moja zimetolewa. Aidha, sekta hii imeendelea kuwa kichocheo cha ukuaji wa sekta mbalimbali zikiwemo kilimo, elimu, mawasiliano, burudani usafirishaji na uzalishaji wa huduma mbalimbali kwa watalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutekeleza mipango ya uendelezaji wa sekta ya utalii kama ilivyoainishwa katika Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/2017 – 2020/2021 na mipango ya kila mwaka wa fedha. Kwa ujumla mipango ya uendelezaji wa sekta inajumuisha utunzaji na uboreshaji wa vivutio vya utalii vilivyopo, uainishaji na uboreshaji wa vituo vipya vya utalii, uboreshaji wa miundombinu ya utalii, uboreshaji wa utoaji wa huduma kwa watalii na kwa umuhimu wa pekee kuongeza mbinu na jitihada za kutangaza utalii wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa upande mwingine Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo katika kutekeleza programu na miradi mbalimbali ya maendeleo ya sekta ya utalii. Kwa mfano, kwa kipindi cha mwaka 2017 – 2022, Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia itatekeleza mradi wa kuboresha utalii Ukanda wa Kusini mwa Tanzania kwa gharama ya takribani Dola za Kimarekani zisizopungua milioni mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua na kuthamini kazi kubwa na ngumu inayofanywa na Askari Wanyamapori wanapotekeleza majukumu yao ya kutoa ulinzi na kusimamia uhifadhi kwa ujumla wa wanyamapori hususani kupambana na ujangili. Aidha, kuanzia mwaka wa Fedha 2016/2017, Serikali imejipanga kuboresha mazingira ya kazi ya Askari Wanyamapori sambamba na watumishi wengine ambapo kwa upande wa Askari Wanyamapori, upatikanaji wa vitendea kazi, uboreshaji wa stahili zao na usimamizi bora zaidi wa utendaji kazi ni miongoni mwa malengo ya Mamlaka ya Wanyamapori (TAWA). Mamlaka hii imeanzishwa tarehe 16 Oktoba, 2015 ili ifanye kazi sambamba na Mamlaka ya Ngorongoro na TANAPA katika kutekeleza lengo kuu la udhibiti wa ujangili nchini.