Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
1961-1995 Session 1 Sitting 1 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 34 2016-11-03

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-
Askari Magereza katika Mji wa Tarime wamekuwa wakilalamika kuwepo kwa mlundikano wa mahabusu ndani ya Gereza la Mji wa Tarime. Hii inatokana na mlundikano wa kesi ndani ya Mahakama ya Wilaya kwa kigezo cha upelelezi kutokamilika:-
(a) Je, kwa nini kesi zenye vigezo vya dhamana watuhumiwa wasipewe dhamana ili kupunguza mlundikano wa mahabusu na gharama kwa Serikali?
(b) Je, nini mkakati mahususi wa Serikali katika kuhakikisha Jeshi la Polisi linamaliza upelelezi kwa wakati ili kuweza kupunguza mlundikano?
(c) Je, ni hatua gani zinachukuliwa kwa Askari Polisi ambao wanawabambikia kesi wananchi na kupoteza nguvu kazi za Taifa kwa kuwafanya wananchi waishi Gerezani?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi nchini, chini ya Kifungu 64 cha Sheria na Mwenendo wa Makosa ya Jinai limepewa mamlaka ya kutoa dhamana kwa baadhi ya makosa kabla washtakiwa kufikishwa Mahakamani. Mara nyingi mahabusu wanaendelea kukaa magerezani licha ya makosa yao kuwa ya dhamana kwa kushindwa kukamilisha masharti chini ya Kifungu 148(5), (6) na (7) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, Sura ya 20 na masharti mengine yanayotolewa na Mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutoa mafunzo ya upelelezi ya muda mfupi na muda mrefu nje na ndani ya nchi ili kuwajengea weledi wapelelezi na kufanya upelelezi kufanyika na kukamilika kwa wakati. Aidha, Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa na Wilaya wanaendelea kuboresha mifumo ya usimamizi wa upelelezi na kukagua mafaili mara kwa mara ili kujionea mwenendo wa kesi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa siyo kweli kwamba Askari Polisi hukumbatia kesi za wananchi. Uhaba wa vitendea kazi vya uchunguzi ambavyo hupatikana Makao Makuu tu, vile ambavyo ni vya kisayansi kuchelewa kupatikana kwa majibu ya uchunguzi wa kisayansi kutoka vyombo vingine, ni baadhi ya sababu ambazo zinafanya baadhi ya upelelezi kuchukua muda mrefu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, iwapo kuna malalamiko dhidi ya Polisi, uchunguzi hufanyika kwa mujibu wa Kanuni ya 103 ya Kanuni za Kudumu za Polisi na Askari akipatikana kwa makusudi akawa na hatia, hatua za kinidhamu na kisheria huchukuliwa dhidi yake.