Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 51 2016-11-04

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL aliuliza:-
Je, ni kwa nini Serikali imekuwa hairudishi katika Halmashauri zetu 30% ya mauzo ya viwanja?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philipo Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara yangu haikuwahi kuwa na utaratibu wa kurudisha asilimia 30 za mauzo ya viwanja kwa Halmashauri, kwa sababu mauzo ya viwanja hufanywa na Halmashauri husika wanapokuwa na mradi wa viwanja katika maeneo yao na Wizara hupokea ada ambazo zinahitajika kisheria katika uandaaji wa hati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 30 ya fedha ambazo zilikuwa zinarejeshwa Halmashauri ni kodi ya ardhi ambapo katika mwaka wa fedha 2015/2016, Wizara ilipeleka mgao wa Sh. 3,541,212,774.01 kwa Halmashauri zote nchini na Halmashauri ya Babati ilipokea jumla ya Sh. 24,138,421.39.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Wizara imekuwa inakumbwa na changamoto kadhaa katika kurejesha asilimia 30 ya fedha za makusanyo. Miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na:-
(i) Halmashauri nyingi kutotuma taarifa za makusanyo kwa wakati ili kuiwezesha Wizara kufanya ulinganisho wa kiasi kilichopokelewa na kile kilichokusanywa.
(ii) Baadhi ya Halmashauri kutumia fedha za makusanyo kabla ya kuziwasilisha kwenye akaunti ya makusanyo ya maduhuli inayosimamiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
(iii) Wizara kupatiwa mgao mdogo wa fedha unavyopokelewa Wizarani kutoka Hazina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, Serikali imeondoa utaratibu wa marejesho ya retention ya asilimia 30 ya makusanyo ya fedha zote zinazoingia katika Mfuko Mkuu wa Hazina. Aidha, Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutaangalia namna bora ya kuweka utaratibu wa utoaji wa fedha kwa ajili ya uendeshaji wa sekta ya ardhi katika Halmashauri zetu.