Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 52 2016-11-04

Name

Anna Richard Lupembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-
Wananchi waliojenga nyumba katika maeneo ambayo hayajapimwa wanapopata kesi hasa kwenye Mahakama ya Wilaya wanatakiwa kutoa Hati au Ofa lakini kwa kukosa nyaraka hizo ndugu au jamaa wanakosa kudhaminiwa:-
Je, Serikali haioni kuwa iko haja ya kupandisha thamani ya makazi ya wananchi hao?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali namba 52 la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli maeneo mengi katika majiji na miji takribani asilimia 70 ya wakazi wake hayana miliki salama na kwa hali hiyo kukosa uhalali wa kutumika kama dhamana kuwadhamini ndugu zao pale wanapokuwa na mashauri katika Mahakama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa ardhi kama rasilimali inayoweza kuwasaidia wanyonge kujikwamua kiuchumi na kutumika kama dhamana katika mashauri ya Mahakama na shughuli nyingine za kiuchumi, Wizara yangu imefanya mambo yafuatayo:-
(i) Kuandaa program ya Kitaifa ya miaka mitano (2015 – 2020) ya kurasimisha makazi yaliyojengwa kiholela na kutoa hati miliki kwa wamiliki wake. Awamu ya kwanza ya urasimishaji wa makazi ambayo imeanza katika Kata za Kimara na Saranga katika Jiji la Dar es Salaam ambapo nyumba au viwanja 6,000 vitapimwa na kumilikishwa kwa wananchi katika kipindi cha miezi sita kuanzia Juni mpaka Disemba, 2016. Awamu ya pili itahusisha upimaji na umilikishaji wa nyumba au viwanja katika Manispaa tano za Jiji la Dar es Salaam za Kinondoni, Ilala, Temeke, Ubungo na Kigamboni) ambapo viwanja 299,000 vitapimwa.
(ii) Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri za Musoma, Tabora, Singida, Kigoma, Ujiji, Sumbawanga na Lindi mwezi Septemba 2016 imefanya tathmini ya maeneo ya urasimishaji ambapo jumla ya viwanja/nyumba 50,200 zimebainishwa kuweza kurasimishwa katika mwaka wa fedha 2016/2017. Kimsingi zoezi hili ni endelevu kwa nchi nzima na litaendelea pia kulingana na upatikanaji wa rasilimali utakavyokuwa unaruhusu.
(iii) Kuandaa progam ya miaka kumi (2015 – 2020) ya kupanga na kumilikisha kila kipande cha ardhi. Program hii ambayo itaratibiwa na Wizara yangu, itahusisha wadau wengine zikiwemo sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la urasimishaji makazi holela litaongeza thamani ya kila kipande cha ardhi kwa kuwapatia wakazi husika hati miliki baada ya kupanga maeneo yao. Aidha, litaongeza ulinzi wa ardhi na kupunguza migogoro ya ardhi na litarahisisha pia utoaji huduma muhimu za kijamii kwa kuainisha maeneo ya huduma na kuhakikisha huduma muhimu zilizokuwa zinakosekana zinapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa tumeshaanza kukabidhi hati katika Mkoa wa Morogoro, Mtaa wa Bingwa Kisiwani ambapo hati 28 zimetolewa na Mwanza eneo la Buhongwa hati 18 zimetolewa. Jumla ya hati miliki 46 zimetolewa kufikia tarehe 30/10/2016 ambazo imekuwa chachu kwa wananchi wengi katika maeneo mengine.