Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 1 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 1 2017-01-31

Name

Omar Abdallah Kigoda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Mjini

Primary Question

MHE. OMARI A. KIGODA Aliuliza:-
Hospitali ya Wilaya ya Handeni inahudumia wagonjwa kutoka Kilindi, Mziha, Wegero na Handeni yenyewe.
Je, ni lini Serikali itaipatia vifaa tiba na wauguzi wa kutosha hospitali hiyo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Abdallah Kigoda, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kutambua mahitaji ya vifaa tiba katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni, Serikali imetenga shilingi milioni 181.9 katika bajeti ya mwaka 2016/2017 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Fedha zote zimeshapokelewa na zimetumika kununulia vifaa tiba vinavyohitajika kusaidia utoaji wa huduma vikiwemo BP machine, vifaa vya kupimia kiwango cha damu, vifaa vya kujifungulia na kupima upumuaji wa watoto, pamoja na kulipia gharama za manunuzi ya jokofu katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Halmashauri imeomba mkopo kutoka Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) ili kununua ultra-sound yenye thamani ya shilingi milioni 75. Halmashauri imeahidi kurejesha fedha zote kupitia makusanyo ya Tele kwa Tele ya Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
Mheshimiwa Spika, mahitaji ya watumishi katika Hospitali hiyo ni 359, watumishi waliopo ni 170 na upungufu ni watumishi 189. Halmashauri imeomba kibali cha kuajiri watumishi 118 katika mwaka wa fedha 2016/2017 ambapo baadhi ya watumishi hao watapelekwa katika Hospitali ya Wilaya. Kati ya watumishi hao walioombwa, watumishi 49 ni wauguzi, watumishi 25 ni madaktari na kada nyingine ni watumishi 44.