Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 33 2017-02-02

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-
Halmashauri ya Nsimbo imekuwa ikipokea wahamiaji toka mikoa mbalimbali ambao ni wakulima na wafugaji na kusababisha kukosa maeneo yenye rutuba.
Je, ni lini Serikali itaongeza maeneo ya vijiji vilivyotangazwa mwaka 1974?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote vilivyoanzishwa mwaka 1974 katika Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, vinapakana na Hifadhi ya Taifa ya Katavi na Msitu wa Hifadhi wa Msaginya, Mulele Hills na Mpanda North East. Misitu hii pamoja na Mbuga ya Katavi iko chini ya usimamizi wa Wizara ya Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi za Taifa zipo kwa mujibu wa Sheria kwa maslahi mapana ya Taifa zima na hairuhusiwi kuendesha shughuli za kilimo na ufugaji katika maeneo hayo yaliyohifadhiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, endapo kuna hoja ya kuongeza eneo la kijiji kwa kumega eneo la hifadhi, kijiji kinatakiwa kwanza kuanza mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa kuainisha takwimu za msingi za idadi ya watu, idadi ya kaya, ukubwa wa eneo lililopo na mahitaji ya ardhi ya ziada.
Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyenye mahitaji ya ardhi kutoka kwenye hifadhi vinatakiwa kujadili suala hili katika Mikutano Mikuu ya Vijiji, Kamati ya Maendeleo ya Kata, Kamati ya Ushauri ya Mkoa na hatimaye maombi hayo kuwasilishwa Wizara yenye dhamana na kuwasilishwa kwa maamuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa wito kwa viongozi wa Vijiji, Wilaya na Mkoa, kuweka utaratibu wa kudhibiti wahamiaji haramu katika maeneo ya mipakani wakiwemo wafugaji wanaoingiza mifugo katika Hifadhi za Taifa.