Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 1 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 8 2016-01-26

Name

Dr. Faustine Engelbert Ndugulile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigamboni

Primary Question

MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE aliuliza:-

Hapa Tanzania kumekuwepo na migogoro mbalimbali ya ardhi kati ya wawekezaji na wananchi, wakulima na wafugaji, hifadhi na wananchi na baina ya wananchi wenyewe:-

(a) Je, Serikali ina mikakati gani ya kupanga matumizi bora na endelevu ya ardhi ili kuondokana na migogoro?

(b) Je, Serikali ina mikakati gani ya kuondokana na tatizo la maendeleo ya miji kutokuendana na kasi ya ukuaji wa miji?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha kuandaa Mpango wa Taifa wa Matumizi ya Ardhi wa mwaka 2013 mpaka 2033. Mpango huu ndiyo kiunzi wa matumizi ya ardhi yaani National Land Use Framework Plan unaotoa maelekezo ya namna ya kupanga maeneo yote nchini kuanzia katika ngazi ya Kanda, Mkoa, Wilaya na Vijiji. Mpango huu umeanza kutekelezwa kupita programu sita za kipaumbele ambazo ni makazi na miundombinu mikuu ya uchumi, kilimo na mifungo, ardhi ya hifadhi na utalii, maeneo ya nishati na madini, mipango ya matumizi ya ardhi kwa ngazi za chini, pamoja na programu ya kuboresha Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi. Kupitia programu hizi, ardhi kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii itategwa na hivyo kuondokana na migogoro baina ya watumiaji mbalimbali wa ardhi. Aidha, Serikali imeandaa programu ya kupanga, kupima na kumilikisha ardhi nchi nzima ili kuondokana na migogoro ya ardhi.

(b) Mheshimiwa Spika, katika miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na ongezeko kubwa la wakazi mijini ambako kumepelekea mamlaka za upangaji na uendelezaji miji kushindwa kutoa huduma za kijamii na kiuchumi kwa kiwango stahiki na hivyo kufanya miji yetu kukua kiholela. Katika kukabiliana na changamoto hizi, Wizara yangu imeendelea kuratibu uandaaji wa mipango kabambe ya Majiji na Miji mbalimbali nchini ambayo itatoa muongozo wa uendelezaji wa miji kwa kuzingatia mahitaji mbalimbali na hivyo kuondokana na tatizo la ukuaji wa miji isiyopangwa. Hadi sasa mipango kabambe ya Majiji ya Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Miji ya Mtwara, Musoma, Iringa, Bariadi, Bagamoyo, Kibaha na Shinyanga iko katika hatua za mwisho za maandalizi na itakamilika kabla ya mwezi Agosti, 2016. Aidha, Mipango Kabambe ya Miji ya Tanga Singida, Tabora, Songea, Morogoro, Sumbawanga, Geita, Njombe na Mpanda ipo katika hatua mbalimbali za maandalizi.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa mamlaka za upangaji ambazo hazina mipango kabambe kutenga fedha katika bajeti zao ili kuharakisha uandaaji wa mipango kabambe na mipango ya kina itakayotoa mwongozo wa uendeleshaji katika miji yao na hivyo kuzuia tatizo la ukuaji wa miji isiyopagwa.