Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 13 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 107 2017-04-27

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO Aliuliza:-
Kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa leseni za udereva katika Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya kutokana na kutokuwepo kwa huduma hiyo. Hali hiyo inapelekea wananchi kupata adha kubwa ya kufuata huduma za leseni Musoma Mjini ambao ni Mkoa mwingine wa Polisi; kutokana na adha hiyo wananchi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali waliamua kujenga na kukamilisha jengo la usalama barabarani:-
(a) Je, ni lini Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya utafungiwa mitambo ya kutoa leseni za udereva ili kuondoa usumbufu uliopo sasa wa kutumia gharama na muda kufuata huduma hiyo Musoma Mjini?
(b) Je, ni lini Ofisi za Mkoa wa Polisi Tarime/Rorya zitajengwa ili kurahisisha utoaji huduma kwa wananchi?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania na Jeshi la Polisi Usalama Barabarani imekuwa ikiboresha huduma za utoaji leseni za udereva na ukusanyaji wa ada za leseni ili kuhakikisha kuwa huduma hizi zinawafikia wananchi bila usumbufu. Serikali kupitia taasisi hizi imefunga mitambo ya kutoa leseni za udereva kila Makao Makuu ya Mkoa ambapo wananchi wote wanaohitaji huduma hizi hufika Mkoani na kuhudumiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufunga mitambo hii kunahitajika maandalizi makubwa ya kifedha na uandaaji wa miundombinu ya mtandao, majengo na rasilimali watu. Kwa sasa, mitambo hiyo imefikishwa hadi kwenye Mikoa ya kikodi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania. Serikali ingependa kufunga mitambo ya kutoa leseni za udereva katika ngazi za Wilaya ikiwemo Wilaya ya Tarime/Rorya. Hata hivyo, kwani gharama za kufunga mitambo hii katika Wilaya zote nchini ni kubwa mno. Serikali inao mkakati wa kufikisha huduma hizi Wilayani ikiwemo Wilaya ya Tarime/Rorya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kipolisi Tarime/ Rorya ni miongoni mwa Mikoa mipya ambayo bado haijajengewa ofisi mpya za kisasa ikiwemo Songwe, Katavi, Simiyu na Geita. Serikali inatambua uhaba huo wa ofisi katika mikoa hiyo na kuna mkakati wa ndani wa kujenga ofisi hizo kwa kutumia rasilimali zilizopo kama nguvu kazi ya wafungwa na kutengeneza matofali ya kujengea ofisi hizo muhimu kwa huduma ya Kipolisi na Idara zingine za Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.