Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 14 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 117 2017-04-28

Name

Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FELISTER A. BURA aliuliza:-
Serikali imeanzisha Benki ya Kilimo kwa lengo la kusaidia wakulima wakubwa na wadogo kupata mikopo ya pembejeo kwa haraka:-
Je, ni lini Benki hiyo itaanza kutoa huduma kwa wakulima wadogo wadogo wa Mkoa wa Dodoma?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Felister Aloyce Bura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Benki ya Maendeleo ya Kilimo ilianza rasmi shughuli zake mwishoni mwa mwaka 2015. Hadi kufikia Desemba 2016, Benki ya Maendeleo ya Kilimo ilikuwa imeshatoa mikopo ya jumla ya Sh. 6,489,521,120/= kwa miradi 20 ya kilimo katika Mikoa ya Iringa, Morogoro na Tanga. Sambamba na utoaji wa mikopo, benki inatoa mafunzo kwa wakulima na hadi sasa imeshafanya mafunzo kwa vikundi 336 vya wakulima wadogo wadogo vyenye jumla ya wanachama 44,400 katika Mikoa ya Iringa, Morogoro na Tanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Mkoa wa Dodoma, Benki imepata nafasi kwa ajili ya kufungua ofisi katika jengo jipya la PSPF ambapo inasubiri kukabidhiwa ofisi hiyo Julai, 2017, baada ya mkandarasi kukamilisha ujenzi. Aidha, benki imeshaanza kutafuta miradi ya kilimo ya wakulima wadogo wadogo yenye sifa za kukopesheka iliyopo katika Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine ya jirani.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kufanikisha azma hii, benki imemwandikia barua Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma kumwomba aipatie miradi mizuri ya kilimo ambayo mkoa unapendekeza Benki iifikirie katika zoezi la kutoa mikopo. Pamoja na hayo, benki inaandaa utaratibu wa mafunzo yatakayotolewa kwa wakulima wadogo wadogo nchi nzima ikianzia na Mkoa wa Dodoma. Ni matumaini ya benki kuwa mikopo kwa wakulima wadogo wadogo na wakati kwenye Mkoa wa Dodoma itaanza kutolewa mwishoni mwa mwaka 2017.