Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 15 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 125 2017-05-02

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Uhitaji wa zao la pareto duniani ni mkubwa sana kiasi kwamba inahitajika kwa takribani tani 18,000 hadi 20,000 katika Soko la Dunia na Tanzania tuna uwezo wa kuzalisha hadi tani 8,000 tukiwa na mazingira rafiki.
(a) Je, ni kwa misingi gani pareto imepangiwa mnunuzi mmoja tu wa kigeni huku ikiwafungia milango wanunuzi wadogo wa Kitanzania?
(b) Je, Serikali inachukua hatua gani kusimamia bei
ya zao hilo ambayo imeporomoka kutoka shilingi 2,400 katika kipindi cha wanunuzi wengi hadi shilingi 1,500 chini ya mnunuzi mmoja?
(c) Je, Serikali ina mkakati gani wa muda mrefu na muda mfupi wa kuwawezesha wanunuzi wadogo wa Kitanzania kuingia kwenye ushindani na wanunuzi wageni?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a),(b) na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Sheria na Kanuni za Pareto zinamtaka kila mnunuzi kuongeza thamani ya pareto kwa kuzidua sumu ya pareto kupata sumu ghafi. Pia mnunuzi anatakiwa kuwa na maabara ya kupima kiwango cha sumu kwenye maua na kuwalipa wakulima kulingana na kiwango hicho cha sumu. Kwa sasa mnunuzi aliyetekeleza masharti hayo ni Kampuni ya Pareto Tanzania. Serikali inasisitiza mnunuzi yeyote kutimiza vigezo vilivyopo katika sheria na kanuni ili kulinda ubora na soko.
Mheshimiwa Spika, bei ya zao la pareto hupangwa katika Mkutano Mkuu wa Wadau ambao ni wa Kisheria na hufanyika kabla ya mwezi Julai kila mwaka kabla ya kuanza msimu mpya. Mkutano huo, huhudhuriwa na wanunuzi na wawakilishi wa wakulima na viongozi wa Halmashauri zinazolima pareto nchini.
Mheshimiwa Spika, Serikali inasisitiza wakulima kuzingatia kanuni za kilimo bora. Kwa mfano, pamoja na bei ya juu kuwa shilingi 2,200 msimu wa 2012/2013 na shilingi 2,700 msimu wa 2014/2015 ubora wa pareto ulikuwa chini ya asilimia moja. Baada ya baadhi ya wakulima kutekeleza kanuni za kilimo bora cha pareto katika msimu wa 2015/2016, ubora ulifikia asilimia 1.8 na bei ya juu kuwa shilingi 2,700.(Makofi)
Mheshimiwa Spika, mkakati wa muda mrefu ni kuendelea kuhamasisha wazawa kujiunga pamoja na kukopa ili wawekeze katika viwanda vya kuongeza thamani ya zao la pareto kufikia kiwango cha crude extract na hatimaye kuingia kwenye ushidani na wanunuzi wa kigeni.