Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 18 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 145 2017-05-05

Name

Faida Mohammed Bakar

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR aliuliza:-
Majukumu ya Mbunge kwa kuzingatia matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 63(3) yameainisha kwa ujumla wake bila kubagua aina ya Ubunge; lakini Sheria Namba 16 ya mwaka 2009 iliyounda Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo (CDCF) imeonesha ubaguzi mkubwa kwa kumtambua Mbunge wa Jimbo pekee ambaye ndiye aliyetajwa na sheria hiyo kama Mwenyekiti wa Kamati ya Usimamizi wa Mfuko huo na kuwatenga Wabunge wa Viti Maalum licha ya kwamba Wabunge wote wanatekeleza majukumu sawa ya kuwatumikia wananchi.
Je, ni lini Serikali itarekebisha sheria hii ili ijumuishe Wabunge wote ikiwemo Wabunge wa Viti Maalum?

Name

Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya Jimbo ulianzishwa mwaka 2009 kwa Sheria Namba 16 ya mwaka 2009 iliyotungwa na Bunge. Fedha za Mfuko wa Jimbo hutolewa katika Majimbo yote ya uchaguzi Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar kwa kuzingatia vigezo maalum vilivyopitishwa kisheria. Vigezo vinavyotumika kugawa fedha za Mfuko wa Jimbo ni idadi ya watu asilimia 45, mgao sawa (pro-rata) kila Jimbo asilimia 25, kiwango cha umaskini asilimia 20 na ukubwa wa eneo asilimia 10.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha za Mfuko wa Jimbo huingizwa moja kwa moja katika account ya Halmashauri na zinasimamiwa kwa taratibu za Sheria ya Fedha isipokuwa Mbunge wa Jimbo ni Mwenyekiti wa Mfuko huo. Kimsingi sheria haina ubaguzi kwa Waheshimiwa Wabunge wa Viti Maalum kwa sababu fedha hizo za Serikali zinatumika kutekeleza miradi ya kipaumbele iliyoibuliwa na wananchi wenyewe kwenye Jimbo husika kwa kuzingatia mahitaji ya Jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na malengo yaliyounda Sheria ya Mfuko wa Jimbo na vigezo vinavyotumika katika kupeleka fedha za Mfuko wa Jimbo, Serikali inaona sheria hiyo inajitosheleza kwa sasa kwa kuzingatia misingi ya uundwaji wake, labda Bunge ambalo ndilo lenye mamlaka ya kutunga sheria litakavyoamua vinginevyo.