Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 32 Defence and National Service Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa 260 2017-05-23

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Primary Question

MHE. KAPT. GEORGE H. MKUCHIKA aliuliza:-
Sheria ya Jeshi la Kujenga Taifa ya Mwaka 1964 (The National Service Act. 1964) imeweka ulazima wa Vijana Watanzania wanaomaliza kidato cha sita kujiunga na mafunzo ya Jeshi la kujenga Taifa kwa mujibu wa Sheria.
(a) Je, katika miaka mitatu iliyopita ni vijana wangapi waliomaliza kidato cha sita kila mwaka na kati yao wangapi walijiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa?
(b) Je, waliojiunga ni asilimia ngapi wa waliotakiwa kujiunga?

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa George Huruma Mkuchika, Mbunge wa Newala Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Sheria ya Jeshi la Kujenga Taifa ya mwaka 1964 imeweka ulazima wa vijana wa Tanzania wanaomaliza kidato cha sita kujiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa Sheria. Hata hivyo, mwaka 1994 Serikali iliyasitisha kwa muda mafunzo hayo na kuyarejesha mwaka 2013 na yameendelea kutolewa hadi sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu za vijana waliohitimu kidato cha sita na kuhudhuria mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa Sheria ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2014, vijana waliomaliza kidato cha sita ni 41,968, kati yao waliojiunga na mafunzo ya Jeshi la kujenga Taifa ni 31,692, ambayo ni sawa na asilimia 75.5.
Mwaka 2015, vijana waliomaliza kidato cha sita ni 40,753, kati yao waliojiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa ni 19,990, ambao ni sawa na asilimia 48.8.
Mwaka 2016, vijana waliomaliza kidato cha sita ni 63,623, kati yao waliojiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa ni 14,747, ambao ni sawa na asilimia 23.2.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zilizopo zinaonesha kupungua kwa idadi ya vijana wanaojiunga na mafunzo hayo muhimu ya Jeshi la Kujenga Taifa. Hali hii imesababishwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na kugongana kwa tarehe za kuanza mafunzo ya vijana kwa mujibu wa Sheria na kufunguliwa kwa vyuo mbalimbali hapa nchini ambapo mihula ya mafunzo huanza.
Hali hii imewafanya vijana wengi walioteuliwa kujiunga na vyuo kukosa nafasi za kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa Sheria. Changamoto nyingine ni uhaba wa miundombinu, rasilimali watu na fedha. Hata hivyo Serikali inaendelea na juhudi za kupata suluhu ya changamoto zilizopo.