Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 27 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 220 2017-05-17

Name

Zaynab Matitu Vulu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYNABU M. VULU aliuliza:-
Kwa sasa kituo kikuu cha mabasi yaendayo mikoani cha Ubungo Jijini Dar es Salaam kimezidiwa uwezo wa kutoa huduma kwa ufanisi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha vituo vingine kikanda ili kuboresha huduma za usafiri wa mabasi yanayoingia na kutoka mikoani?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaynabu Matitu Vulu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ipo katika mipango ya kuanzisha vituo vingine mbadala vya mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani baada ya kituo kikuu cha mabasi cha Ubungo kuzidiwa uwezo wa kutoa huduma kwa ufanisi kama ifuatavyo:-
(a) Kituo cha mabasi Mbezi Luis, chenye eneo la mita za mraba 68,000 kitahudumia mabasi yatokayo katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini (Mbeya, Rukwa, Iringa, Ruvuma na Njombe); Kanda ya Ziwa (Mwanza, Shinyanga, Kagera, Mara, Geita na Simiyu); Kanda ya Kati (Dodoma, Singida na Manyara); Kanda ya Magharibi (Tabora, Kigoma na Katavi) na nchi za jirani za Malawi, DRC, Burundi, Rwanda, Zimbabwe na Zambia.
(b) Kituo cha mabasi cha Boko Dawasa chenye eneo la mita za mraba 63,121 kitahudumia mabasi yatokayo mikoa ya Kanda ya Kaskazini na Mashariki (Arusha, Kilimanjaro na Tanga) na nchi za jirani za Kenya na Uganda.
(c) Kituo cha mabasi cha Kanda ya Kusini, kitatafutiwa eneo sehemu ya Kongowe kwa ajili ya kuhudumia mabasi yatokayo Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma.