Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 51 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 420 2017-06-20

Name

Raisa Abdalla Mussa

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RAISA ABDALLAH MUSSA aliuliza:-
Wapo wanawake ambao wamefungwa kwenye magerezani wakiwa na watoto wachanga/wadogo ambao bado wanahitaji uangalizi au huduma za mama zao.
(a) Je, Serikali imejipanga vipi katika kuwanusuru watoto hao ambao hawana hatia?
(b) Je, Serikali haioni kuwa inavunja haki za binadamu kwa kuwaweka gerezani watoto hao wasio na makosa?
(c) Je, Serikali inaweza kulipa Bunge takwimu za wanawake waliokinzana na sheria na wamefungwa kwa miaka mitano iliyopita?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Raisa Abdallah Mussa, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a), (b), na (c) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo mazingira ambayo watoto wadogo na watoto wachanga huingia gerezani wakiwa wameambatana na mama zao kutokana na mama zao kufungwa gerezani au kuingia mahabusu, ama mama zao kuingia wakiwa wajawazito na baadae kujifungua gerezani. Watoto hao hupokelewa na kuruhusiwa kuwepo gerezani na mama zao kwa mujibu wa Kifungu cha 144(1) cha Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Kanuni 728 ya Kanuni za Kudumu za Jeshi la Magereza za mwaka 2003.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kuruhusu watoto kuwa na mama zao magerezani unatokana na kuzingatia maslahi ya mtoto kama inavyohimizwa katika Mkataba wa Kimataifa wa Haki ya Mtoto (The Convention of Rights of the Child) na mikataba mbalimbali ya kikanda inayohusiana na haki za mtoto. Kwa kuwa mtoto mchanga huwa bado ananyonya, hivyo himaya stahiki ya malezi na makuzi ya awali huwa ni ya mama yake. Hata hivyo Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 imetoa nafasi kwa mtoto ambae mzazi wake wake yuko katika ukinzani wa sheria kuweza kupata malezi mbadala ambayo yanazingatia mahitaji yote ya mtoto kama ilivyo kwa mtoto yeyote yule chini ya uangalizi wa uongozi wa magereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2012 hadi mwaka 2016, idadi ya wanawake waliofungwa magerezani kutokana na kukinzana na sheria ilikuwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2012 ni 364, mwaka 2013 ni 321, mwaka 2014 ni 373, mwaka 2015 walikuwa ni 334 na mwaka 2016 ni 616. Hivyo kufanya jumla yake wote kuwa ni 2008.