Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 51 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 421 2017-06-20

Name

Elias John Kwandikwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ushetu

Primary Question

MHE. ELIAS J. KWANDIKWA aliuliza:-
Miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na mauaji ya wazee na walemavu wa ngozi kutokana na sababu mbalimbali.
(a) Je, ni idadi ya watu wangapi waliopoteza maisha katika Jimbo la Ushetu kwa kipindi cha mwaka 2010 hadi 2015?
(b) Je, mauaji ya makundi haya yanapungua au yanaongezeka katika Jimbo la Ushetu?
(c) Je, Serikali imeshirikisha vipi jamii kupiga vita mauaji haya, vikiwemo vikundi vya dini, walinzi wa jadi (sungusungu) na uongozi wa kimila Jimboni Ushetu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elias John Kwandikwa, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mwaka 2010 wazee waliouawa walikuwa wawili, mwaka 2011 wazee wanne, mwaka 2013 wazee watano, mwaka 2014 wazee waliouawa walifikia sita, mwaka 2015 walikuwa wawili, mwaka 2016 wawili na mwaka 2017 alikuwa ni mzee moja. Kwa hiyo, jumla ya wazee ambao wamepoteza maisha katika kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwaka 2010 hadi 2017 ni wazee 22 katika Jimbo la Ushetu. Kwa upande wa walemavu wa ngozi, katika kipindi hicho hakuna mlemavu aliyeuawa wala kujeruhiwa Jimboni Ushetu ila kwa nchi nzima kwa kipindi cha miaka 2010 mpaka 2017 walemavu wa ngozi waliouawa walikuwa ni sita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa mauaji ya makundi haya katika miaka ya karibuni yanapungua kutokana na misako iliyofanywa ya kuwakamata waganga wa kienyeji ambao wanapiga ramli chonganishi na kuchochea imani za kishirikina.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukomesha mauaji haya, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwemo kushirikiana na taasisi mbalimbali zisizo za Kiserikali ndani na nje ya Jimbo hilo katika kutoa elimu ya ukatili huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikishirikiana na jamii na taasisi za kidini, vikundi vya ulinzi jamii ndani na nje ya Jimbo la Ushetu kwa kuwapa elimu wananchi ili kudhibiti maujai hayo ya kikatili.